WAZEE WA MILA WAWASAKA VIONGOZI WA DINI KUZUNGUMZIA AMANI YA KUDUMU

TARIME

WAZEE wa mila kutoka katika koo 13 za kabila la wakurya, wilayani Tarime mkoani Mara,wameanza mazungumzo na viongozi wa kanisa la Anglikana Tanzania dayosisi ya Tarime ya kusaka amani ya kudumu.
 
Wazee hao pia wameahidi kusaidiana na Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Tarime na Rorya katika kudhibiti vitendo vya uhalifu na uhalifu katika wilaya hiyo.
 
Wazee hao wameyasema hayo katika kongamano ambalo limeitishwa na Askofu wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Tarime Dk. Mwita Akiri kwenye Kituo cha Maendeleo ya Kilimo Mogabiri, wilayani humo limehudhuriwa pia na Kamanda wa Polisi mkoa wa Kipolisi wa Tarime/ Rorya, Kamishna Msaidizi Justus Kamugisha.
 
Aidha wazee hao wa mila pamoja na wachungaji wa kanisa hilo la Anglikana, wameahidi kutoa ushirikiano utakaosaidia kudumisha amani na usalama katika kukabiliana na uhalifu.
 
Akifungua kongamano hilo, Askofu Dk. Mwita amewasisitizia wazee hao wa mila kuhakikisha wanasimamia haki, ambayo itazaa amani na hatimaye kuleta maendeleo badala ya wao kuwa chanzo cha kuchochea migogoro na uhasama dhidi ya koo nyingine.
 
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Tarime na Rorya ACP Justus Kamugisha, amesema jeshi lake limekuwa likishirikiana na wazee wa mila katika kurejesha amani wilayani humo, kwa kudhibiti mapigano ya koo na koo, wizi wa mifugo ulioambatana na mauaji pamoja na kilimo cha bangi.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo