Muonekano wa Bwawa la kuzalisha umeme mto Ijangala
Askofu Dkt Alex Malasusa (Kulia) akiweka jiwe la msingi mradi wa kuzalisha umeme wa Ijangala
Ujenzi wa mradi wa kufua umeme katika mto Ijangala (Ijangala Mini Hydropower Project) wilayani Makete mkoani Njombe umefikia asilimia 92.13 mpaka sasa na unatarajiwa kukamilika na kukabidhiwa ifikapo Desemba 31, 2023
Katika shughuli ya uwekaji jiwe
la Msingi mradi huo lililofanyika kwenye eneo mradi huo unatekelezwa katika
kijiji cha Masisiwe, Mkurugenzi wa Udiakonia Dayosisi ya Kusini Kati Mdiakonia
Elikana Kitahenga akisoma taarifa ya ujenzi wa mradi huo amesema muda wa
kukabidhi mradi huo Tanesco waliosainishana nao haukutosha ambapo ilitakiwa
wakabidhiane Juni 26, 2022 hivyo kutokana na changamoto mbalimbali ambazo
hazikuepukika mradi huo bado haujakamilika ili ukabidhiwe
Amesema wamewasilisha Tanesco
ombi la kuongezewa muda wa kazi na hivyo makabidhiano mapya yamepewa muda hadi
Desemba 31, 2023
“Makadirio ya awali ya uwekezaji
wa mradi huu yalikuwa ni jumla ya shilingi bilioni 3.34, kwa sasa gharama
zimepanda na kufikia jumla ya shilingi bilioni 4.59 na hii ni kwa kadri ya
hesabu hadi mwisho wa mwezi wa nne, kanisa kupitia kampuni yake kama mjenzi wa
mradi huu ina wajibu sasa wa kutafuta tofauti ya shilingi bilioni 1.24 ambayo
kwa kweli ni pengo ili kukamilisha kabisa mradi huu na kulipa wakandarasi wote”
amesema Kitahenga
Baba Askofu wa Kanisa la kiinjili
la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Mashariki na Pwani Dkt Alex Malasusa
ambaye allikuwa Mgeni rasmi kwa niaba ya Mkuu wa KKKT Askofu Fredrick Shoo
ameoneshwa kufurahishwa na kanisa kutekeleza mradi huo ambao amesema unawapa
ufahari na umewaondolea woga
Amesema mara nyingi watu wengi
hawawezi kutekeleza miradi kwa sababu ya woga lakini wale wanaothubutu kama
Dayosisi ya kusini kati kipekee watu wa udiakonia wameonesha uthubutu na kanisa
siku zote linataka watu wanaothubutu
“Mungu akizungumza na wewe juu ya
mradi anza, usijidharau, nani alijua kwamba wadiakonia wanaweza wakakaa na
wakaweza kubuni mradi kama huu, leo liwe fundisho kwa miradi yetu mingi
tusiukumbatie umasikini, name niungane na wenzangu kuishukuru sana serikali
nikisema serikali ni pamoja na vyombo vyake vyote, kwa jinsi ambavyo wameenda
hatua kwa hatua ili mradi huu uweze kuonekana na ukielekea kukamilika” amesema
Askofu Malasusa
“Niseme huu ni mradi ambao
umenifurahisha sana REA ninatamani sana hata baadaye niweze kujua mawasiliano
ya kukutana nao ni watu ambao tunahitaji kama kanisa kuwaunga mkono sana kwa
sababu watu walio wengi katika nchi hii wako vijijini na watu walisahauliwa kwa
muda mrefu ni hawa walioko vijijini, na wadiakonia tuwashukuru kwa
kutuunganisha na REA” amesema Dkt Malasusa
Kwa upande wake Askofu wa
Dayosisi ya Kusini Kati Wilson Sanga amesema mradi huo wa umeme sio wa kwanza
katika dayosisi hiyo kwani ina mradi wa umeme kupitia hospitali ya kanisa
Bulongwa ambao unahudumia tarafa ya Bulongwa na Magoma na pia wanamradi
mwingine mdogo ambao upo katika kata ya Lupila ambao unahudumia sehemu ya
vijiji vya kata ya Lupila na bado upo katika hatua za ujenzi
“Tunaamini Bwana akipenda
tutakuwa nawe au wakati mwingine katika mradi kama huu, karibu sana baba Askofu
unayemuwakilisha Mkuu wa kanisa lakini mkuu wa kanisa mstaafu sisi tumebarikiwa
kwamba baada ya kustaafu kwako tumepata baraka katika mradi huu” amesema Askofu
Sanga
Mwakilishi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hamisi Mrope amesema mwaka 2010 walipokea ombi kutoka
kwenye mradi wa umeme Ijangala na kuombwa ufadhili wa kufanya upembuzi yakinifu
ambapo wao kama wakala baada ya kuwezeshwa na serikali waliwapatia fedha dola
elfu 87 ili kufanya upembuzi yakinifu, kuchangia milioni 426 kujenga laini, na
kuchangia dola laki mbili na elfu kumi na moja kwa ajili ya wataalamu wakiwemo
waliofanya upembuzi yakinifu katika mradi huo
Amesema wao kama wakala wana
wajibu wa kuwawezesha wazalishaji wadogo kwa kuwaunganisha na benki za biashara
ambazo zinatoa mikopo ambapo waliwaunganisha na benki ya TIB na wakapewa mkopo
wa dola laki nne (Milioni 920) ili kuendeleza mradi huo.