Picha 11 za Mradi wa Umeme mto Ijangala Makete, Askofu Malasusa afunguka

Muonekano wa Bwawa la kuzalisha umeme mto Ijangala

Askofu Dkt Alex Malasusa (Kulia) akiweka jiwe la msingi mradi wa kuzalisha umeme wa Ijangala

Ujenzi wa mradi wa kufua umeme katika mto Ijangala (Ijangala Mini Hydropower Project) wilayani Makete mkoani Njombe umefikia asilimia 92.13 mpaka sasa na unatarajiwa kukamilika na kukabidhiwa ifikapo Desemba 31, 2023

 

Katika shughuli ya uwekaji jiwe la Msingi mradi huo lililofanyika kwenye eneo mradi huo unatekelezwa katika kijiji cha Masisiwe, Mkurugenzi wa Udiakonia Dayosisi ya Kusini Kati Mdiakonia Elikana Kitahenga akisoma taarifa ya ujenzi wa mradi huo amesema muda wa kukabidhi mradi huo Tanesco waliosainishana nao haukutosha ambapo ilitakiwa wakabidhiane Juni 26, 2022 hivyo kutokana na changamoto mbalimbali ambazo hazikuepukika mradi huo bado haujakamilika ili ukabidhiwe

 

Amesema wamewasilisha Tanesco ombi la kuongezewa muda wa kazi na hivyo makabidhiano mapya yamepewa muda hadi Desemba 31, 2023

 

“Makadirio ya awali ya uwekezaji wa mradi huu yalikuwa ni jumla ya shilingi bilioni 3.34, kwa sasa gharama zimepanda na kufikia jumla ya shilingi bilioni 4.59 na hii ni kwa kadri ya hesabu hadi mwisho wa mwezi wa nne, kanisa kupitia kampuni yake kama mjenzi wa mradi huu ina wajibu sasa wa kutafuta tofauti ya shilingi bilioni 1.24 ambayo kwa kweli ni pengo ili kukamilisha kabisa mradi huu na kulipa wakandarasi wote” amesema Kitahenga

 

Baba Askofu wa Kanisa la kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Mashariki na Pwani Dkt Alex Malasusa ambaye allikuwa Mgeni rasmi kwa niaba ya Mkuu wa KKKT Askofu Fredrick Shoo ameoneshwa kufurahishwa na kanisa kutekeleza mradi huo ambao amesema unawapa ufahari na umewaondolea woga

 

Amesema mara nyingi watu wengi hawawezi kutekeleza miradi kwa sababu ya woga lakini wale wanaothubutu kama Dayosisi ya kusini kati kipekee watu wa udiakonia wameonesha uthubutu na kanisa siku zote linataka watu wanaothubutu

 

“Mungu akizungumza na wewe juu ya mradi anza, usijidharau, nani alijua kwamba wadiakonia wanaweza wakakaa na wakaweza kubuni mradi kama huu, leo liwe fundisho kwa miradi yetu mingi tusiukumbatie umasikini, name niungane na wenzangu kuishukuru sana serikali nikisema serikali ni pamoja na vyombo vyake vyote, kwa jinsi ambavyo wameenda hatua kwa hatua ili mradi huu uweze kuonekana na ukielekea kukamilika” amesema Askofu Malasusa

 

“Niseme huu ni mradi ambao umenifurahisha sana REA ninatamani sana hata baadaye niweze kujua mawasiliano ya kukutana nao ni watu ambao tunahitaji kama kanisa kuwaunga mkono sana kwa sababu watu walio wengi katika nchi hii wako vijijini na watu walisahauliwa kwa muda mrefu ni hawa walioko vijijini, na wadiakonia tuwashukuru kwa kutuunganisha na REA” amesema Dkt Malasusa

 

Kwa upande wake Askofu wa Dayosisi ya Kusini Kati Wilson Sanga amesema mradi huo wa umeme sio wa kwanza katika dayosisi hiyo kwani ina mradi wa umeme kupitia hospitali ya kanisa Bulongwa ambao unahudumia tarafa ya Bulongwa na Magoma na pia wanamradi mwingine mdogo ambao upo katika kata ya Lupila ambao unahudumia sehemu ya vijiji vya kata ya Lupila na bado upo katika hatua za ujenzi   

 

“Tunaamini Bwana akipenda tutakuwa nawe au wakati mwingine katika mradi kama huu, karibu sana baba Askofu unayemuwakilisha Mkuu wa kanisa lakini mkuu wa kanisa mstaafu sisi tumebarikiwa kwamba baada ya kustaafu kwako tumepata baraka katika mradi huu” amesema Askofu Sanga

 

Mwakilishi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hamisi Mrope amesema mwaka 2010 walipokea ombi kutoka kwenye mradi wa umeme Ijangala na kuombwa ufadhili wa kufanya upembuzi yakinifu ambapo wao kama wakala baada ya kuwezeshwa na serikali waliwapatia fedha dola elfu 87 ili kufanya upembuzi yakinifu, kuchangia milioni 426 kujenga laini, na kuchangia dola laki mbili na elfu kumi na moja kwa ajili ya wataalamu wakiwemo waliofanya upembuzi yakinifu katika mradi huo

 

Amesema wao kama wakala wana wajibu wa kuwawezesha wazalishaji wadogo kwa kuwaunganisha na benki za biashara ambazo zinatoa mikopo ambapo waliwaunganisha na benki ya TIB na wakapewa mkopo wa dola laki nne (Milioni 920) ili kuendeleza mradi huo.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo