Polisi wamewakamata wanawake wanne na daktari mmoja wa kiume kuhusiana na wizi wa mtoto kutoka kwa mama aliyejifungua katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Bungoma.
Katika kisa hicho cha Disemba 5, 2022, Mercy Chebet, mkazi wa Chepyuk, alikuwa amejifungua watoto mapacha, mvulana na mtoto wa kike, kwa njia ya upasuaji. Lakini alishangaa alipokabidhiwa mtoto wa kike pekee baada ya kujifungua. Mama huyo alitaka kujua aliko mtoto mwingine kwani, wakati wa kliniki za kabla ya kuzaa picha ya ultrasound scan ilionyesha alikuwa amebeba mapacha.
Kulingana na taarifa ya polisi iliyothibitishwa na TUKO.co.ke, Chebet alisema kuwa daktari aliyemhudumia alipuuzilia mbali madai yake na kusisitiza kuwa alizaa mtoto mmoja pekee. Isitoshe daktari huyo alimtolea stakabadhi zote zinazohusiana na ujauzito wake. Baada ya uchunguzi, makachero wa Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) katika kaunti ya Bungoma walimpata Joseline Simiyu akiwa na mtoto mchanga aliyeibwa katika mjini Bungoma.
Simiyu alikuwa pamoja na Irene Atieno, Robai Namiti, Rodah Namiti na daktari Joseph Owola ambao wote walikamatwa. Watano hao watafikishwa mahakamani leo, Jumatatu, Februari 13, kujibu mashtaka ya ulanguzi wa watoto. Polisi pia waliagiza usimamizi wa Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Bungoma kurekodi taarifa zinazoeleza jinsi mtoto huyo alipotea.
Chanzo:Tuko