Serikali kutoa milioni 100 kutatua tatizo la maji Mlondwe

Katibu Mkuu Wizara ya Maji Mhandisi Antony Sanga akizungumza alipofanya ziara ya kikazi katika kata ya Mlondwe.

Na Edwin Moshi, Makete


Serikali imesema itatoa kiasi cha shilingi milioni 100 kwa ajili ya kutatua tatizo la maji Mlondwe wilayani Makete mkoani Njombe ambalo limepelekea kero kwa wananchi wa eneo hilo

 

Akizungumza baada ya kufanya ziara ya kikazi kijijini hapo Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji Mhandisi Antony Sanga baada ya kujionea changamoto za mradi huo amesema serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan haina shida ya fedha hivyo kwa kuwa eneo hilo lina shida ya maji amewasiliana na Waziri wa maji Jumaa Aweso, kabla ya wiki hii kumalizika serikali itawaletea shilingi milioni 100 kwa ajili ya kutatua changamoto ya maji

 

Katibu Mkuu Sanga amemuagiza Meneja wa RUWASA wilaya ya Makete Mhandisi Innocent Lyamuya kujipanga kupokea fedha hiyo kwa ajili ya ujenzi wa mradi wa maji Mlondwe ili kuondoa changamoto hiyo huku akihimiza mradi huo ujengwe kwa kasi ili ukamilike kwa wakati na wananchi waanze kupata huduma ya maji

 

"Hata huu mradi muujenge kwa kasi, haya matenki muendelee nayo lakini wakati huo yale mabomba m-diverge (myachepushe)wananchi wapate maji, kwa hiyo ndugu zangu kina mama wa Mlondwe, waheshimiwa viongozi wote wa Mlondwe,ndugu zangu wananchi wenzangu wa Mlondwe wiki ijayo (wiki hii) tunawaletea fedha mtakapoombwa ushirikiano basi muwe tayari ili ndani ya muda mfupi basi muanze kujenga mradi huu wa maji ambao mmechukua muda mrefu ninyi kunufaika nao" amesema Mhandisi Sanga

 

Awali Meneja wa RUWASA wilaya ya Makete Mhandisi Innocent Lyamuya akitoa taarifa kwa Katibu Mkuu ya Mradi wa Maji Mlondwe amesema mradi huo ulitegemewa kugharimu shilingi Bilioni 2 na milioni 84 na mpaka sasa umegharimu shilingi Bilioni 1.5 ambapo amesema walipokuwa wanaingiza maji kwa watu, mabomba yaliyopo kwa kuwa ni ya zamani yalishindwa kuhimili na yapasuka hali iliyochangia kuwepo na upotevu wa maji

 

"Sasa hii imechangia kuwepo na changamoto ya upotevu wa maji pamoja na kwamba mradi umeleta maji ya kutosha sasa kuna upotevu wa maji mengi huku njiani kutokana na ile miundombinu kuwa ya zamani hivyo hiyo ni changamoto kubwa ya huo mradi" - Amesema Mhandisi Lyamuya

 

Amesema kwa kuwa mradi huo una bakaa ambayo imebaki na kwamba wameshafanikisha maeneo mengi wanaomba kwamba kwenye njia za usambazaji waweze kupatiwa fedha ili waweze kumalizia sehemu zilizobaki ikiwemo kubadilisha mabomba ya zamani na kuweka mabomba mapya ili wananchi wapate maji kwenye maeneo yao

 

"Mh Katibu Mkuu kwa kifupi sana hiyo ndiyo taarifa ya huu mradi ni mradi mzuri sana na umetekelezwa vizuri matenki makubwa lakini changamoto iliyopo mkuu ni hiyo kwenye maeneo ya njia za usambazaji" amesema Meneja huyo wa RUWASA

Mkuu wa wilaya ya Makete Juma Sweda amesema wana imani kwamba tatizo la majia Mlondwe sasa litakwisha na hivyo kunusuru hali ya ndoa za baadhi ya watu zilizokuwa zipo kwenye migogoro kutokana na changamoto ya maji

 

Naye Mwenyekiti wa Chama cha mapinduzi (CCM) Wilaya ya Makete Clemence Ngajilo amesema wao kama chama walifaya ziara na kujionea changamoto ya maji inayowakabili na kuahidi kulishughulikia hivyo ujio wa Katibu Mkuu huyo ni ishara tosha kwamba serikali inawajali wananchi wake

 

Diwani wa kata ya Mlondwe Alphonce Salimo ameshukuru kwa hatua hizo zilizochukuliwa na serikali na kukiri kuwa walikuwa wakisumbuliwa na mvujo wa maji hivyo wanaimani kwamba tatizo hilo litakwenda kumalizika huku mmoja wa wakazi wa kijiji hicho akishukuru kwa hatua hizo ambazo zitawapunguzia adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta huduma ya maji.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo