Mkurungenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) Mhandisi Hassan Saidy amesema Mtu anayetumia nishati ya mkaa na kuni kupikia kwa siku moja ni sawa na Mtu anayevuta sigara 300 hivyo ni hatari kwa afya na usalama wa mazingira.
Ameyasema hayo katika eneo la Ifakara Mkoani Morogoro wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi wa kimkakati wa kupoza umeme wa Ifakara unojengwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya.
"Watu wengi hasa maeneo ya vijijini wanatumia nishati ya kuni na mkaa kupikia na kubwa zaidi kwa vijijini ni kuni ile ya mafiga matatu na unavuta moshi wa kutosha sana na tuliambiwa Mtu anayepika kwa kuni na mkaa kwa siku moja ni sawasawa na Mtu aliyevuta sigara 300 sasa unaweza kuona athari yake ni kiasi gani"