MKURUNGEZI Msaidizi wa Kinga na Meno kutoka Wizara ya Afya, Dk.Baraka Nzoba amesema asilimia 76.5 ya watu wazima Tanzania wameoza meno kutokana na kutopiga mswaki huku watoto waliooza meno nchini ni asilimia 31.1.
Amesema sababu kubwa ya tatizo la kulegea, kutoboka na kuoza kwa meno linalowakabili watoto na watu wazima katika jamii ni kutokana na kutopiga mswaki vizuri ikiwa ni pamoja na matumizi ya sukari iliyosindikwa inayopatikana katika vyakula mbali mbali.
“Kawaida mtu anapaswa kupiga mswaki angalau mara mbili kwa siku, asubuhi anapoamka na usiku anapotaka kulala, sasa Watanzania wengi kupiga mswaki inaonekana ni kipengelee, wengi wanapata matatizo ya kinywa kwa kutopiga mswaki.” amesema
Kauli ya Dk Nzoba imekuja baada ya Shirika la Afya Dunia (WHO), kutoa ripoti yake juzi Novemba 20, 2022 ikionyesha karibu nusu ya watu duniani sawa na asilimia 45 au watu bilioni 3.5 wanaugua magonjwa ya kinywa, huku watu watatu (3) kati ya wanne (4) walioathirika wakiishi katika nchi za kipato cha chini na cha kati.