Katika hali isiyokuwa ya kawaida, Mama mmoja amedaiwa kushambuliwa kwa kipigo huku akitishiwa maisha na mme wake kwa madai ya kumwomba fedha ya matumizi ya familia katika mtaa wa Geita Road kata ya Nyatukala Wilayani Sengerema Mkoani Mwanza.
Akizungumzia tukio hilo mama aliyeshambuliwa kwa kipigo amesema kuwa pindi anapomwomba fedha za matumizi mme wake amekuwa akiambulia kipigo, huku akilazimika kuishi maisha ya kulala njaa na mtoto wake mwenye umri wa mwaka 1 na miezi mitatu kwa kukosa chakula.
Baadhi ya wananchi wa mtaa huo wamesikitishwa na tukio hilo na kuiomba serikali kumchukulia hatua kali za kisheria mwanaume huyo anayedaiwa kufanya kitendo hicho cha kikatili.
Naye afisa ustawi wa jamii katika kituo cha afya cha Sengerema Consolatha Magaka amesikitishwa na kulaani vikali tukio hilo na kuahidi kumkamata mwanaume huyo na kumchukulia hatua kali za kisheria ili kukomesha matukio ya ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake yanayoendelea kushika kasi wilayani humo.