“Tunamsubiri Sista Mkuu wa Maria Consolata , Sista Jane ambaye yupo safarini akitokea Dar es Salaam kuja Iringa na atakapofika le oleo tutapanga taratibu za mwisho za mazishi yao” alisema.
Kasesela alisema kabla ya mazishi yao, mapacha hao wataagwa katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Ruaha (Rucu) walikokuwa wakisoma shahada ya ualimu.
Aliomba kama kuna ndugu wa mapacha hao popote pale nchini wajitokeze kushiriki mazishi hayo ili kuwapa faraja katika safari yao ya mwisho.
“Hatuna taarifa za ndugu wowote toka tumewafahamu mapacha hao, tunachojua wamekuwa wakilelewa kanisa Katoliki kwa msaada wa wadau mbalimbali kwa maisha yao yote,” alisema.
Wakati huo huo, Kasesela amemshukuru Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dk John Pombe Magufuli kwa rambirambi yake ya Sh Milioni 5 aliyotoa kuomboleza kifo cha mapacha hao.
Nao wanafunzi wa chuo cha RUCu waliokuwa wakisoma na pacha hao wamesema wameupokea msiba huo kwa masikitiko makubwa.
“Baada ya kupokea taarifa hizi, chuo kilikuwa kama kimemwagiwa maji. Hakuna aliyeamini taarifa hizo japokuwa ukweli ndio huo. Mungu azilaze roho zao peponi,” alisema mmoja wao aliyejitambulisha kwa jina la Rose.
Maria na Consolata walizaliwa wilayani Makete mkoani Njombe mwaka 1996.
Walisoma shule ya Msingi Ikonda Makete na kuhitimu na kufaulu mtihani wa darasa la saba mwaka 2010, kisha wakajiunga na shule ya Maria Consolata iliyopo Kilolo mkoani Iringa ambapo walihitimu kidato cha nne mwaka 2014.
Baada ya hapo walijiunga na shule ya Sekondari ya Udzungwa wilani Kilolo walipohitimu kidato cha sita mapema mwaka 2017 na wote kufaulu kwa kupata daraja la pili na hatimaye Septemba 2017 wakajiunga na Chuo Kikuu cha Katoliki cha Ruaha (Rucu) walipokuwa wakisomea fani ya ualimu mpaka mauti inawafika.
