Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe amegoma kumpa pole Mbunge wa Mbeya Mjini , Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ pamoja na mwenzie Emmanuel Masonga baada ya kutoka gerezani kwa madai kuwa viongozi wote wa upinzani kwa sasa ni wafungwa watarajiwa.
Zitto Kabwe ameandika katika ukurasa wake wa mtandao wa Twitter kwamba amefurahi kuona wako huru huku akiamini kuwa kukaa kwao gerezani kumewaongezea ari ya kupigania Demokrasia nchini.
“Nafurahi kuwa Mbunge Mbeya Mjini Ndg. Joseph Mbilinyi (Sugu) na mdogo wangu Emmanuel Masonga wametoka Gerezani! siwapi pole, maana katika nyakati za Udikteta wapinzani wote ni wafungwa watarajiwa. Naamini kukaa kwao gerezani kumewaongezea zaidi ari ya kupambania Demokrasia pana ya Nchi yetu.Watawala mjue sasa kuwa vifungo vya Uonevu, kututishia Maisha na hata kutupiga risasi havita turudisha nyuma kwenye kupigania demokrasi ya nchi yetu.“ameandika Zitto Kabwe.
Sugu ameachiwa huru leo Mei 10, 2018 kutoka gereza la Ruanda, Mbeya alipokuwa akitumikia kifungo cha miezi mitano kwa makosa ya uchochezi.
