Mkuu wa Polisi wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Mrakibu Mwandamizi wa Jeshi la Polisi, Bw. Nico Mwakasanga ameamuru kukamatwa kwa askari polisi aliyejulikana kwa jina la Bw. Mbunda na kuwekwa ndani kwa uchunguzi baada ya baadhi ya wananchi kutoa malalamiko kwa mkuu wa mkoa Mh.Christina Mndeme kufanyiwa vitendo vya unyanyasaji na askari huyo.
Wakitoa malalamiko hayo kwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mh. Christina Mndeme ambaye kwa mara ya kwanza amefanya ziara ya kikazi wilayani Tunduru tangu kuteuliwa kwake Octoba kushika wadhifa huo, baadhi ya wananchi hao wa Tunduru wamesema askari huyo amekuwa akiwanyanyasa kwa kuwabambikiza kesi na wakati mwingine kukamata wananchi wakiwa kwenye shughuli za uzalishaji mali akiwaita wazururaji.
Akijibu malalamiko hayo ya wananchi, Mkuu wa Polisi wa wilaya ya Tunduru, Mrakibu Mwandamizi wa jeshi la Polisi, Mwakasanda amesema ameshaagiza askari Polisi huyo akamatwe popote alipo na kuwekwa ndani kwa uchunguzi zaidi.
Hata hivyo Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Mh, Christina Mndeme amewaonya askari polisi kuacha tabia ya kubambikizia kesi wananchi na badala yake watende haki huku akiwataka wananchi wasiogope kutoa taarifa polisi endapo wanafanyiwa vitendo hivyo ili hatua zaidi zichukuliwe.
