Maiti za watu wa wawili zimekutwa zikiwa zimetupwa ndani ya ziwa Victoria katika eneo la rest manispaa ya Musoma huku chanzo cha tukio hilo kikiwa bado hakijafahamika.
Kamanda wa polisi mkoa wa Mara , Jaffari Mohamed amezungumza na mwandishi wa blog hili kuwa miili hiyo bado haijatambuliwa na kwamba polisi wanaendelea na uchunguzi zaidi juu ya tukio hilo.
Alisema kuwa bado miili hiyo haijafahamika kuwa ni watu kutoka nchi gani kwa maelezo kwakuwa eneo ilipopatikana miili hiyo kuna mkondo wa maji kasi ndani ya ziwa na kwamba upo uwezekano wa miili hiyo kuwa imetokea nchini Kenya au nchini.
Aliongeza kuwa maiti moja yenye jinsi ya kiume imepatikana ikiwa imeharibika ambapo alifafanua kuwa hawezi kutoa taarifa zaidi kwa vile yupo nje ya mkoa na kwamba uchunguzi wa kipolisi unaoendelea.
kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Mara Adam Malima amethibitisha kutokea kwa tukio hilo ambapo alisema kuwa atakuja kutoa ufafanuzi wa kina juu ya suala hilo baada ya kupata taarifa ya uchunguzi kutoka katika vyombo husika.
"Nitazungumza na vyombo vya habari hivi karibuni kulitolea suala hili ufafanuzi naomba mnipe muda vyombo husika vimalize uchunguzi kwanza ila nataka kusisitiza kuwa ingawa kuna tukio Hilo lakini Hali ya ulinzi na usalama ya mkoa wetu iko salama kabisa" alisema .
Wakizungumzia tukio hilo baadhi ya wananchi ambao hawakutaka majina yao kutajwa walisema kuwa zaidi ya miili minne ukiwepo mwili wa mwanamke mmoja imeopolewa katika eneo Hilo Kuanzia wiki iliyopita.
mwananchi mmoja alisikika akisema hali imekuwa ya kutisha sasa kwakuwa kama watu wanauwawa na kutupwa majini hatufahamu hawa watu wametokea wapi au wamefanya kosa gani mpaka wameuwawakinyama.
