Maji yaadimika Rombo, Ndoo Moja ya maji inauzwa 1000

Wananchi wa kijiji cha Mengwe chini wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro  wanakabiliwa na tatizo la maji kwa miaka mitatu  na wanalazimika kununua ndoo au debe moja kwa shs.1000/= kutoka kwa  vijana wa boda boda walioligeuza tatizo hilo kuwa biashara  yao.

Wakizungumza na mwandishi wa ITV ambayo ilishuhudia baadhi ya maeneo yakiwa na mabomba  yameota  kutu na koki za maji kuzingirwa na buibui wananchi hao wamesema, kilio chao ni cha muda mrefu lakini hakijapatiwa ufumbuzi.

Bi Anna Shayo amesema,yeye ni mteja wa maji wa kampuni ya maji ya Kilwater lakini bomba lake halijatoa maji tangu mwaka 2013 na wazazi kwa jumla  wanaogopa kuwatuma watoto wao kwenda kutafuta maji umbali mrefu kwa hofu ya kubakwa njiani

Wakazi wengine wa kijiji hicho Bw Benardin Asenga na Evaline Shayo  wameiomba serikali iwajengee mtandao mwingine wa maji katika kijiji hicho kutoka maeneo ya milimani ili kulipatia ufumbuzi wa kudumu tatizo hilo ambalo ni tofauti na vijiji jirani ambavyo vinapata maji

Meneja mkuu wa kampuni ya maji ya Kilwater Bw Prosper kessy amekiri kuwepo kwa tatizo hilo ingawa si kwa kijiji kizima ambalo limesababishwa na uharibifu wa miundombinu ya maji uliyofanywa na baadhi ya wananchi ambao utafanyiwa ukarabati.

Hata hivyo mkuu wa wilaya ya Rombo Bi Agness Hokororo amesema,tatizo hilo ni kubwa kutokana na maji kidogo  yanayozalishwa na Kilwater na serikali imeanza mchakato wa kuanzisha mamlaka ya maji ambayo itasimamiwa na Wizara ya maji ili kutosheleza mahitaji ya wananchi wa wilaya ya Rombo.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo