‘Polisi mkikuta mtu kwenye msitu piga, haki za binadamu waje kwangu’ - RC Makonda

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ameliagiza Jeshi la Polisi kuwagonga na kuwapiga wahalifu wowote wakiwamo majambazi pindi wanapowakamata. 

Akizungumza wakati wa kuaga miili ya askari watatu kati ya wanne wa Jeshi la Polisi waliouawa wiki hii katika tawi la benki ya CRDB lililopo Mbande wilayani Temeke jijini Dar es Salaam, Makonda alisema jambazi atakapokutwa popote iwe msituni iwe wapi agongwe na apigwe. 

Alisema alipopata taarifa ya vifo vya askari hao wanne alifungua pazia za madirisha nyumbani kwake na kuwaangalia askari wanaolinda na kulia kwa uchungu na kwamba usiendelezwe ukichaa wa haki za binadamu kwani ni uendawazimu ambao hauwezi kuvumilika. 

“Kamanda Sirro (Simon) mimi ndiyo mkuu wako wa mkoa nasema ukikamata hao watu popote gonga, piga na watu wa haki za binadamu wakija waambie waje kwangu, hatuwezi kukaa kwenye mkoa ambao haupo salama,” alisema Makonda aliyedai hana maneno mazuri ya kusema kwa sababu hakuumbwa kumfurahisha mtu, bali anafanya kazi ya Mungu na wakati wake ukiisha ataondoka.

 “Kama kuna haki za binadamu nataka haki za askari wangu kwanza. Kama hao watu wa haki za binadamu wapo nataka kuona wakiandamana kukilaani kitendo hiki, ”alisema Makonda. 

Hata hivyo, kauli hiyo ya Makonda imepingwa na wanasheria wakidai kuwa mwenye haki ya kutoa hukumu ya kuadhibiwa au kutoadhibiwa ni mahakama na si mtu mwingine. 

Wakili kutoka Crax Law Partners, Hamza Jabir alisema kisheria mtu yeyote anapokamatwa kwa tuhuma yoyote anakuwa ni mtuhumiwa hivyo hakuna mwenye haki ya kumhukumu. 

Alisema baada ya kufanyika uchunguzi wa kubaini tuhuma hizo kama za kweli au la, anapelekwa mahakamani na mahakama ndiyo pekee yenye haki ya kuhukumu kama kwa kosa alilokutwa nalo ana haki ya kufungwa, kupigwa au kuuawa.

 “Kutoa hukumu bila kufuata taratibu za kisheria ni kuingilia uhuru wa mhimili wa sheria ambao unajitegemea, ”alisema Jabir. 

Wakili wa kujitegemea Juma Nassor alisema anayetuhumiwa kwa kosa lolote ikiwamo kuua, adhabu yoyote anayopaswa kupewa, mwenye haki ya kuidhinisha na kuitamka adhabu hiyo ni mahakama. 

“Inatambulika nchi inaendeshwa kisheria, hivyo ni sheria pekee inayopaswa kuhukumu ili uipate sheria lazima tuhuma zozote zifanyiwe uchunguzi, mhusika apelekwe mahakamani, halafu mahakama kwa kuangalia viele- lezo ndiyo itatoa hukumu ya aina yoyote iwe kuuawa, kunyongwa au vinginevyo, ”alisema Nassoro.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo