Waziri awamu ya 4 awachana Kikwete, Makinda

ALIYEKUWA Waziri wa Maliasili na Utalii katika Serikali ya awamu ya nne, Ezekiel Maige Amedai kuwa kitendo cha Serikali yao chini ya Rais Jakaya Kikwete kufuata kasi ya upepo unakovuma na uonevu wa Spika Anne Makinda dhidi yake ndiyo chanzo cha yeye kuenguliwa uwaziri kwa kashfa ya vitalu vya uwindaji na usafirishaji wa wanyama hai mwaka 2012.

Maige aliyeshika nafasi ya unaibu waziri mwaka 2008 hadi 2010 akiwa na Waziri Shamsa Mwangunga na kisha kuwa waziri kamili kuanzia Novemba 27, 2010 hadi Mei, 2012, alisema hadi wakati akijiuzulu, alisema ushahidi wa anachokisema ni ukweli kuwa hakuna mahala alikopewa nafasi ya kujieleza kuhusiana na tuhuma hizo.

Alisema cha kusikitisha, ni ukweli kwamba hatua za kumuwajibisha zilichukuliwa kutokana na mazingira ya wakati huo ya “kufuata upepo” unakovuma na pia kunyimwa kwake fursa ya kujieleza bungeni na aliyekuwa Spika wa Bunge la 10, Makinda.

Alisema kutokana na yote hayo, ndipo alipojikuta akipoteza uwaziri na hadi sasa amebaki na siri nzito moyoni kuhusiana na mambo hayo na pia vitendo vya ujangili.
Maige aliondolewa uwaziri na Rais Kikwete baada ya taarifa ya Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, kumtuhumu kuwa alihusika katika kugawa vitalu vya uwindaji kwa kampuni hewa 16. Aliponzwa pia na uuzaji wa wanyama hai wakiwamo twiga. 

"Bahati mbaya, sisi tuliosimamia sheria tuliondolewa kwa hila. Na bahati mbaya, kwa mazingira ya wakati ule, upepo ukivuma sana unakwenda hivyo hivyo… Ila hivi sasa (chini ya Rais John Magufuli) mambo yamebadilika… kuna usimamizi wa sheria," alisema Maige.

MAKINDA ALIVYOMPONZA
Akielezea kile kilichotokea kabla ya kuachia uwaziri, Maige alisema Makinda alishiriki kwa kiasi kikubwa katika kuondolewa kwake uwaziri kutokana na kile anachodai kuwa spika huyo mstaafu alimkandamiza kwa kutompa muda wa kujitetea bungeni baada ya tuhuma kadhaa kuelekezwa kwake kuhusiana na ugawaji wa vitalu vya uwindaji.

Alisema kabla ya kuondolewa, aliomba apewe fursa ya kuelezea ukweli wa suala hilo, lakini kwa bahati mbaya mazingira kuhusiana na jambo hilo yalijaa harufu ya rushwa na hujuma zilienea dhidi yake hadi bungeni ambako mwishowe hakupata nafasi hata ya kusikilizwa.

"Nilisema bungeni kwamba jambo lolote linalowasilishwa bungeni ni lazima liwe limepitia kwenye kamati. Na huko kwenye kamati ni lazima majadiliano yawe yamekamilika… nilisema yote yaliyojadiliwa bungeni sikuwahi kuitwa na kamati kujibu tuhuma zinazoelekezwa,"alisema Maige na kuongeza:

"Bungeni nikasema, Mheshimiwa Spika, utaratibu hauruhusu hili jambo kujadiliwa maana sijaitwa kwenye kamati… lakini Spika kwa sababu alikuwa na vionjo vyake, ana malengo yake, alisema kamati inaruhusiwa kufanya kazi kama inavyopenda, wewe changia kama mchangiaji.”

Maige aliongeza kuwa baada ya hapo, alifanya jitihada za kuzungumza na mawaziri wenzake, hasa aliyekuwa akishughulikia Sera, Uratibu na Bunge ili asaidiwe kupata nafasi ya kutosha ya kujieleza bungeni lakini jitihada zake hizo pia hazikufanikiwa. 

"Nikasema tena na mawaziri wenzangu, nikimzungumzia Waziri wa Sera, Uratibu na Bunge, nikamwambia usimame usaidie hili suala maana mimi hapa sizungumzi kama Maige, ninazungumza kama Waziri wa Serikali… naomba uliombe Bunge lisitishe mjadala ili nikaandae majibu kama Waziri. Nilipewa dakika 10 za kuchangia kama mchangiaji wa kawaida," alisema.

"Sijaona Waziri, tena mlengwawa tuhuma, anachangia kwa dakika kumi. Zimekuja skendo za ajabu ajabu kama Escrow, Waziri husika amepewa zaidi ya saa moja na dakika 20, anaeleza msimamo wa Serikali. Lakini mimi nilipewa dakika kumi, nilijaribu kueleza (lakini) muda sikupata,"alisema.

chanzo: nipashe


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo