Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema kimesema hakitarusu Mkutano
Mkuu Maalumu wa Chama cha Mapinduzi unaotarajia kufanyika tarehe 23
Julai mwaka huu kwa ajili ya kumkabidhi uongozi Mwenyekiti wa chama
hicho Dk John Pombe Magufuli kutokana na Jeshi la Polisi kutumia nguvu
kutawanya mikutano ya chama hicho na kuzuia mahafali ya wanafunzi wa
vyuo vikuu.
Katibu Mkuu wa Baraza la vijana Chadema taifa Bw.Julius Mwita
ameyasema hayo baada ya Jeshi la Polisi kuzuia mahafali ya kuwatunuku
vyeti wanachama wa vyuo vikuu mkoani Kilimanjaro.
Amesema kitendo kinachofanywa na Jeshi la Polisi kutumia nguvu
kuzuia mikutano ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA ni
kukandamiza Demokrasia hapa nchini na kuwataka vijana kutokata tamaa.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu Taifa (Zanzibar) Salum Mwalimu
amesema wanasikitishwa na kitendo kinachofanywa na Jeshi la Polisi
kutumia nguvu kutawanya mikutano ya chama hicho hapa nchini.
Akielezea mazingira ya kuzingirwa na Jeshi la Polisi Mwenyekiti wa
Bazara la vijana Chadema mkoa wa kilimanjaro Bw.Dikson Kibona amesema
walishangaa kuwaona wakizingirwa huku wakipewa amri ya kutawanyika la
sivyo watatawanyishwa kama hawatatii amri.
