Zoezi la kuwaondoa kwenye nyumba za serikali wadaiwa sugu
linalofanywa na wakala wa majengo (TBA) mkoa wa Mwanza kwa ushirikiano
na kampuni ya udalali ya Yono Auction Mart, limeingia dosari baada ya
mmoja wa wapangaji wa nyumba hizo eneo la Mkuyuni A, jijini Mwanza
kutembeza mkong’oto uliosababisha zoezi hilo kusitishwa.
Zoezi hilo lililokuwa likisimamiwa na askari polisi wawili wenye
silaha, limeingia nuksi baada ya mpangaji huyo ambaye ni askari polisi
wa kitengo cha upelelezi wilaya ya Nyamagana Fabian Jumapili kufika
nyumbani kwake akitumia Defender ya polisi na kuanza moja kwa moja
kutembeza kipigo kwa wafanyakazi wa kampuni ya Yono Auction Mart ambao
walikuwa wakiendelea na kazi ya kutoa nje vyombo vyake vya ndani.
Miongoni mwa watu walioshuhudia tukio hilo lililotokea majira ya
saa sita mchana ni Bi. Esther Joseph na Asha Omar ambao wameeleza
changamoto za utekelezaji wa zoezi hilo.
Afisa wa kampuni ya Yono Auction Mart, Habariki Mhina ambaye
amejeruhiwa mdomoni wakati wa vurugu hizo amesikitishwa na kitendo
kilichofanywa na mpangaji huyo.
Mhandisi Sobe Makonyo ni Kaimu Meneja wa wakala wa majengo mkoa wa
Mwanza anaeleza hatua zitakazochukuliwa mara ya baada ya mdaiwa huyo
kukaidi agizo la serikali kwa kuanzisha vurugu zilizopelekea kusitishwa
kwa zoezi hilo.
