Zoezi la kubomoa jengo lenye ghorofa 16 lililopo katikati ya jiji la Dar es salaam limekamilika kabla ya muda ambapo jumla ya siku 46 zimetumika kukamilisha zoezi hilo badala ya siku 90 zilizotakiwa kubomolea jengo hilo.
Akizunguza kwenye eneo la ubomoaji mkurugenzi wa manispaa wa Ilala Isaya Mgulumi amesema zoezi hilo limetekelezwa na mkandarasi mzalendo kwa gharama ya bilioni 1na limekamilika bila madhara yoyote hali ambayo inaonyesha wakandarasi wa ndani wana uwezo mkubwa wa kiutendaji wanachotaki ni kusimamiwa kwa karibu.
Jengo hilo pacha lililopo mtaa wa Indira Ghandi limevunjwa kufuatia kuanguka kwa jengo lingine liliokuwapo mita chache kutoka katika jengo hilo ambalo nalo lilijengwa ghorofa 16 badala ya ghorofa nane. Jengo hilo liliporomoka na kusababisha vifo vya watu 34 july 23 mwaka 2013.
Pamoja na kuvunjwa kwa jengo hilo wamiliki wa jengo hilo, Mkandarasi, Mkaguzi wa majengo pamoja na maafisa wa ardhi na manispaa walioidhinisha ujenzi huo walifikishwa mahakamani huku mmiliki wa jengo hilo akitakiwa kulipa gharama zote za ubomoaji wa jengo hilo.