Mwenyekiti wa kijiji wilayani Makete ajiuzulu....vitisho vya Imani za kishirikina vyatajwa

Mwenyekiti akitangaza rasmi kujiuzulu.

Mwenyekiti wa kijiji cha Lupalilo kata ya Lupalilo wilayani Makete mkoani Njombe Bw. Victon Sanga amejiuzulu rasmi nafasi hiyo jana mchana kwenye mkutano uliofanyika kijijini hapo

Hatua hiyo inatokana na sababu mbalimbali alizozieleza katika barua yake aliyoiandika kwa na kuwasilishwa kwenye mamlaka za kijiji hicho hivi karibuni

Katika barua hiyo iliyosomwa mbele ya wananchi waliofika kwenye mkutano huo na kaimu afisa mtendaji wa kata hiyo Bw. Mwatima Mbilinyi imeeleza kuwa sababu za yeye kujiuzulu ni kwenda jijini Mbeya kutafuta maisha hali itakayosababisha kuwepo nje ya kijiji hicho kwa muda mrefu na hivyo atashindwa kuyamudu majukumu yake ya kila siku

Amesema yeye pamoja na wajumbe wa halmashauri ya kijiji walimshauri na kumuomba kwa muda mrefu abadilishe uamuzi wake wa kujiuzulu lakini mwenyekiti huyo alikataa na kushikilia msimamo wake wa kujiuzulu

Mwenyekiti aliyejiuzulu Bw. Victon Sanga amesema pamoja na aliyoyaeleza kwenye barua ya kujiuzulu, ameongeza kuwa ameshindwa kumudu majukumu yake ya uenyekiti kwa kuwa kila anachokifanya yeye kinaonekana kibaya kwa wananchi

“baba wa taifa Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kama unaona majukumu uliyopatiwa au kukabidhiwa huyawezi basi huna budi kujiuzulu ili kuwapa nafasi hiyo wengine au mwingine anayeweza aifanye, sasa mimi nimejipima nikaona niiache kwa sababu siiwezi, lakini pia ndugu zangu nao wamenishauri kiiache na watanifadhili katika maisha mengine huko Mbeya” amesema Bw. Sanga

Wananchi waliokuwepo kwenye mkutano huo baadhi yao walimpongeza kwa uamuzi aliouchukua huku wengine wakisikitishwa na kitendo chake cha kujiuzulu kwa kuwa kinakwamisha kazi za maendeleo katika kijiji hicho

“Huyu kijana tulimchagua kwa kishindo tukijua atatusaidia lakini leo anajiuzulu, hivi sisi wana Lupalilo tutapiga hatua kweli? Hapa kijijini kuna wazee wenye mdomo sana, naomba waache mdomo, huyu mwenyekiti ana mengi sana moyoni hapa anaogopa kuyasema, wengine wamemtishia kuwa tuone kama usiku utalala, hapa anaogopa kuyasema, tuache mdomo na maneno kama hayo jamani” amesikika mwanamke mmoja akisema katika mkutano huo bila kujitambulisha jina lake

Mwingine amesema “Huwezi kumlazimisha ng’ombe kunywa maji sana sana utamfikisha mtoni tu, kama mwenyekiti amesoma alama za nyakati na kuona kuwa hawezi kazi basi hatuwezi kumlazimisha”

Kutokana na nafasi hiyo kuachwa wazi ulifanyika uchanguzi wa kumpata mwenyekiti wa kijiji atakayeongoza kwa muda hadi hapo mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Makete atakapoitisha uchaguzi mdogo, na Bw Method Pella akachaguliwa kuwa mwenyekiti wa muda kwa kura 65 dhidi ya Regina Ido aliyepata kura 3

Mwenyekiti huyo ameomba ushirikiano kutoka kwa wananchi ili wafanye maendeleo ya kijiji chao huku akikemea wale wote wenye maneno ya vitisho waache tabia hiyo mara moja


Diwani wa kata hiyo ya Lupalilo Mh. Imani Mahenge ameahidi kutoa ushirikiano kwa kiongozi huyo aliyechaguliwa na kuwataka wananchi kuwa na mshikamano ili kwa pamoja wafanye shughuli za maendeleo katika kijiji chao
 Mwananchi wa Lupalilo akichangia hoja ya mwenyekiti kujiuzulu

 Diwani wa kata ya Lupalilo Mh Imani Mahenge akizungumza neno kufuatia kujiuzulu kwa mwenyekiti
 kaimu Afisa mtendaji wa kata Bw. Mbilinyi akisema machache kufuatia uamuzi huo wa mwenyekiti
 Babu Jota akichangia hoja

 Wengine walisikitishwa na uamuzi wa mwenyekiti wao kujiuzulu
 Wananchi wakipiga kura kumchagua mwenyekiti wa muda
 Wakimpongeza mwenyekiti wa muda aliyechaguliwa
 Mwenyekiti wa muda aliyechaguliwa akiwashukuru wananchi kwa kumchagua


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo