Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi ameacha sintofahamu kwenye wizara hiyo baada ya kusita kutamka maneno ya kuzindua Halmashauri ya 11 ya wapima ardhi katika hafla iliyofanyika kwenye ukumbi wa wizara hiyo.
Hatua ya Waziri kutotamka uzinduzi rasmi, umetokana na kushuhudia viongozi wa Halmashauri hiyo yenye jukumu la kusajili wapima ardhi na wathamini katika kusimamia taaluma na mwenendo wa utendaji katika masuala ya kupima ardhi ni watendaji wakuu katika wizara hiyo.
Akizungumzia mkanganyiko huo, Waziri Lukuvi amesema haiwezekani yakawepo mazingira ya kutenda haki ikiwa viongozi wenye jukumu la kusimamia Halmashauri hiyo ili iweze kusimamia na kuondoa migogoro katika sekta ya ardhi ndio hao hao watendaji wakuu katika wizara hiyo.
Kutokana na hali hiyo, Waziri amependekeza sheria ya kuanzisha halmashauri hiyo ibadilishwe ili kuwaondoa watendaji hao ambao miongoni mwao wanatuhuma za kuhusika na migogoro ya ardhi ili chombo hicho kiongozwe na watu kutoka nje ya serikali.
Wajumbe wapya wa Halmashauri hiyo inaongozwa na Justo Lyamuya kama Mwenyekiti na Katibu ni Nassor Duduma ambao wote ni watendaji katika wizara hiyo