Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha
Mapinduzi (CCM), Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amepokea kwa mshtuko
mkubwa na huzuni nyingi taarifa za kifo cha ghafla cha Mheshimiwa
Kepteni John Damian Komba, Mbunge wa Jimbo la Nyasa, Mjumbe wa
Halmashauri Kuu ya taifa ya CCM na msanii hodari sana wa kizazi chake.
Katika salamu zake za rambirambi kwa Spika wa Bunge, Mheshimiwa
Anne Semamba Makinda na Katibu Mkuu wa CCM, MheshimiwaAbdulrahman
Kinana, Mheshimiwa Kikwete amesema: “Nimepokea kwa mshtuko mkubwa na
huzuni nyingi taarifa za kifo cha ghafla cha Mheshimiwa Kepteni John
Komba, ambacho nimejulishwa kuwa kimetokea mchana wa leo, Jumamosi,
Februari 28, 2015, kwenye Hospitali ya TMJ, Dar es Salaam.”
“Kwa hakika, sina maneno ya kutosha kuelezea kwa fasaha hasara
ambayo taifa letu na chama chetu kimepata kutokana na kifo cha Kepteni
Komba. Taifa letu limepoteza hazina kubwa na mtu muhimu.
Nimejua Kepteni Komba kwa muda mrefu sana,nimefanya naye
kazi, Alikuwa msanii ambaye kiwango chake cha usanii kilikuwa
hakipimiki, alikuwa na sifa kubwa za uongozi,alikuwa mpenzi, mzalendo na
mtu mwaminifu sana kwa taifa lake na katika jambo lolote
aliloliamini.,”amesema Rais Kikwete katika salamu hizo na kuongeza.