Radi Yaua Watu Watano wa Familia Moja huko Shinyanga......Wanne kati Yao Walikuwa ni Wanafunzi

WATU watano wa familia moja wakiwemo wanafunzi wanne wamekufa papo hapo kwa kupigwa radi wakiwa shambani katika Kijiji cha Manungu kata ya Uyogo, Halmashauri ya Ushetu wilayani Kahama, mkoani Shinyanga.
 
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Kahama, Leonard Nyadaho, kwa niaba ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, watu hao walipigwa na radi Februari 28, mwaka huu na kufariki papo hapo kutokana na mvua kubwa iliyokuwa ikinyesha.
 
Nyadaho alisema mvua hiyo iliyoanza kunyesha juzi jioni katika kijiji cha Manungu kitongoji cha Izengwe. Alisema mvua hiyo iliwakuta wananchi hao wakiwa mbugani wakipanda mpunga ndipo walipopigwa na radi na kufariki.
 
Aliwataja marehemu hao kuwa ni Paulina Williamu (28), Magreth Mayunga (13), Herena Mayunga (14), Flora Mathias (13) na Veronica Mathias (14), wote wanafunzi wa Shule ya Msingi Manungu.
 
Mashuhuda walisema marehemu hao waliamka asubuhi na kwenda shambani kupanda mpunga, wakiwa huko ghafla lilitanda wingu zito ndipo mvua iliyoambatana na radi ilipoanza kunyesha.
 
Walisema mvua hiyo kubwa iliyokuwa imeambatana na upepo mkali ilikuwa na muungurumo wa radi wa mara kwa mara. Walisema ilinyesha muda mfupi na ilipokatika walisikia mayowe yakitokea walipokuwa watu hao.
 
"Baada ya kwenda shambani tulikuta wote hao wameshafariki," alisema mmoja wa mashuhuda hao.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo