Chadema kuanza elimu ya mpigakura, SASA KUZINDUA OPARESHENI MAALUMU

Mbunge wa Ubungo, John Mnyika.
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kinatarajia kuzindua operesheni ya kutoa elimu ya mpigakura nchi nzima, itakayoitwa Mkoa kwa Mkoa.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Tanzania Bara, John Mnyika, alisema chama hicho kimeona Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), haijatoa elimu ya kutosha.

Alisema Chadema itaanza rasmi kutoa elimu hiyo mkoani Njombe, ambako uandikishaji wa Daftari la Kudumu la Mpigakura unatarajiwa kuanza, na operesheni hiyo itazinduliwa na Mwenyekiti wa Taifa wa Chadema, Freeman Mbowe.

Mnyika alisema kwa kuwa Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva alitoa hamasa kwa wanasiasa kutoa elimu hiyo, Chadema itaanza rasmi utoaji elimu Njombe na kutaka Jeshi la Polisi kutoingilia kwa kuwa wanafanya jambo la kikatiba.

Kuingilia uandikishaji Alipoulizwa kuhusu kutoa taarifa kwa Polisi, Mnyika alisema walitoa taarifa kuhusu mikutano ya kutoa elimu hiyo, lakini Polisi walijibu kuwa hiyo ni mikutano ya kisiasa na itaingilia uzinduzi wa uandikishaji wa Daftari la Kudumu la Wapigakura.

Uzinduzi huo unatarajiwa kufanyika wiki hii na mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, ambaye yuko katika ziara ya kikazi katika mikoa ya Iringa na Mbeya.

Hata hivyo, Mnyika alisema masuala hayo hayaingiliani na hayahatarishi usalama wa nchi, kauli inayoonesha kuwa chama hicho hakikubaliani na tahadhari ya Polisi.

Maandalizi tayari Uandikishaji wa wapigakura katika Daftari la Kudumu la Mpigakura kwa kutumia mfumo mpya wa teknolojia ya kielektroniki ya BVR (Biometric Voters Registration), unatarajiwa kuanza rasmi mkoani Njombe kesho.

Akizungumza juzi Dar es Salaam, Jaji Lubuva alisema vifaa vinavyohitajika mkoani humo vimeshawasili na kwa kuanza wataandikisha wananchi wenye sifa katika mji mdogo wa Makambako.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, Paulo Malala, alisema wamejipanga vizuri na walishapata mafunzo kuanzia ngazi ya kata hadi mkoa kutoka kwa maofisa na wataalamu wa Nec.

“Mafunzo tumepata na hata maopereta wa BVR, walishafundishwa jinsi ya kutumia mashine hizo na kwa kweli kama wananchi watajitokeza kama tulivyopanga, ni wazi tutamaliza kazi hiyo na muda unatosha,” alisema Malala.

Akizungumza kwa nyakati tofauti katika mikutano ya hadhara juzi mkoani Iringa, Pinda aliwataka Watanzania kwa ujumla wao, kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Mpigakura, ili wawe na uhalali wa kuchagua viongozi wanaowataka wakati ukifika.

“Tupo katika hatua za mwisho za kuanza uandikishaji kwa kutumia teknolojia mpya ya kielektroniki ya BVR (Biometric Voters Registration) na mimi mwenyewe nitafanya uzinduzi mkoani Njombe,” alisema.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo