WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda amepiga marufuku ukarabati wa maabara za
zamani za shule za sekondari na kusisitiza kwamba ni lazima zijengwe
mpya kama ambavyo Serikali ilielekeza.
Alitoa agizo hilo jana mchana, wakati akizungumza na mamia ya wakazi
wa Kata ya Ilula, baada ya kukagua ukarabati wa maabara za sayansi
kwenye Shule ya Sekondari Ilula, wilayani Kilolo, mkoani Iringa.
“Mmefanya ukarabati kwenye jengo lililojengwa zaidi ya miaka 20
iliyopita. Kuna chumba nimekuta ni kidogo mno sababu hakiendani na
maelekezo ya sasa... chumba kimoja kimepasuka ukuta, hapana! Mkuu wa
Mkoa kama kuna nyingine ya aina hii kazi isiendelee.
“Huu ukarabati mliofanya ni kinyume na maelekezo ya Serikali ya
kutaka zijengwe maabara mpya. Tulisema zijengwe maabara mpya, ili zidumu
kwa miaka mingi kidogo. Kuna chumba dari iko chini kwa sababu ujenzi ni
wa zamani.
Ujenzi wa sasa mapaa yako juu zaidi ili kuruhusu hewa ya kutosha.
“Ningeweza kusema vunjavunja, lakini haitakuwa haki kwa sababu kuna
fedha za watu zimetumika... kwa sasa yatatuhifadhi kwa muda kidogo,
lakini haya majengo hayatadumu hata kidogo,” alisema.
Waziri Mkuu pia alikataa kuahidi mchango alioombwa achangie na
kuwaeleza kwamba atakuwa tayari kuchangia ujenzi wa jengo jipya na siyo
ukarabati, kwani huo utakuwa ni upotevu wa fedha.
Majengo aliyooneshwa Waziri Mkuu Pinda, yalijengwa mwaka 1995 na
yalikuwa yakitumika kama maabara kwenye sekondari hiyo. Alimtaka Mkuu wa
Mkoa wa Iringa, Amina Masenza asimamie watu wake ili ujenzi wa maabara
ukamilike kwa muda uliopangwa.
Mkoa huo unahitaji maabara 72 na zilizokamilika ni maabara tano tu
huku nyingine 53 zikiwa kwenye hatua mbalimbali za ujenzi na 13 bado
ziko kwenye msingi na moja iko kwenye lenta.
Awali akitoa taarifa mbele ya Waziri Mkuu, Mtendaji wa Kata ya Ilula,
Titus Katemo alisema Shule ya Sekondari Ilula ilijenga maabara zake
mwaka 1995 kwa nguvu za wananchi na zilikuwa zikitumika kipindi chote
hicho.
Alisema ili kuendana na matakwa ya Wilaya, ukarabati wa vyumba vitatu
ulianza Novemba 15, mwaka jana kutokana na vyumba hivyo kutumiwa na
watahiniwa wa kidato cha nne wa mwaka 2014 kwenye mitihani ya vitendo.
“Makisio ya gharama za ukarabati wa vyumba vitatu yalikuwa Sh milioni
38.29 na tunatarajia ukarabati utakamilika ifikapo Machi 30, 2015,”
alisema na kumuomba Waziri Mkuu awaunge mkono kwa mchango kwani kasi ya
wananchi kuchangia imekuwa ndogo.
Waziri Mkuu anaendelea na ziara yake wilayani Kilolo jana alitarajiwa
kukagua mradi wa umwagiliaji wa Nyanzwa na kuzungumza na wananchi
kwenye mkutano wa hadhara