MAHAKAMA ya Mkoa wa Tabora i m e m h u k u m u Mwinjilisti wa Kanisa
la Menonite Ipuli Manispaa ya Tabora, kifungo cha miaka 30 jela baada ya
kupatikana na hatia ya ubakaji wa msichana wa miaka 16.
Akitoa hukumu hiyo jana, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Mkoa wa Tabora,
Joctan Rushwela alisema kifungo hicho kiwe fundisho kwa watu wengine
wenye tabia kama hizo.
Aliyetiwa hatiani kwa kosa la kubaka msichana huyo (jina
tunalihifadhi ) ni Furaha Muhama (49), mkazi wa Misha Manispaa ya Tabora
baada ya kupatikana na hatia ya makosa mawili.
Hakimu Rushwela alisema kutokana na ushahidi uliotolewa mahakamani
hapo, hakuwa na shaka yoyote ndio maana mahakamani ikafikia uamuzi wa
kutoa kifungo hicho kwa mshitakiwa huyo.
Hakimu huyo alisema kwamba kitendo kilichofanywa na mwinjilisti huyo
kwa muumini wake ni kinatishia amani waumini, ambao watakosa imani na
watoa mahubiri.
Alisema kwamba kitendo kama hicho hakiwezi kuvumilika na mtandao wa
sheria hasa Mahakama kutokana na vitendo vya aina hiyo kukithiri katika
jamii.
Mahakama hiyo ilitoa hukumu kwa makosa mawili, ambapo kosa la ubakaji
kifungo miaka 30 na kumtorosha mtu kwenye himaya ya wazazi kifungo
miaka 5, lakini makosa yote yanakwenda na kifungo kitakuwa miaka 30
jela.
Licha ya kutolewa kwa hukumu huyo, mshitakiwa hakuonesha kuumizwa na
kosa hilo hata baada ya kutakiwa kusema chochote, alisema atakata rufaa
tu hakimu huyo atakapotoa hukumu yake.
Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo, mwendesha mashitaka wa Serikali
aliomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali kwa mshitakiwa huyo ili aweze
kujutia kosa alilolifanya.
Awali mwendesha mashitaka wa serikali, Iddy Mgeni aliiambia mahakama
hiyo kwamba Aprili 24 mwaka huu katika kijiji na Kata ya Ibambo wilaya
ya Uyui mkoani hapa, mshitakiwa alikamatwa kwa makosa mawili ya ubakaji
na kumtorosha mtu kwenye himaya ya wazazi wake.
credits kwa habari leo
