Kardinali Pengo afichua siri ya ugonjwa wake


Claudia Kayombo
ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, amefichua siri ya kupona maradhi yaliyokuwa yakimsumbua kwa muda wa zaidi ya mwaka mmoja sasa.

Alisema alikaa chini ya msalaba wa Yesu Kristo akimwomba naye alifanyia huruma kwa kumponya.

Pia, aliwashukuru maaskofu wasaidizi wake, Eusebius Nzigilwa na Titus Mdoe kwa kufanya kazi vizuri wakati akiwa katika matibabu.

Mwadhama Pengo alitoa kauli hiyo jana Dar es Salaam, wakati akitoa neno la shukrani baada ya Ibada ya Misa takatifu aliyoadhimisha kwenye Kanisa Kuu la Kiaskofu la Mtakatifu Yosefu, ambalo ni makao makuu ya jimbo hilo.

Pamoja na mambo mengine, ibada hiyo ilikuwa ni kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa kutimiza miaka 70, tangu alivyozaliwa.

“Katika kipindi hicho, namshukuru Mungu kwa kuwa amenionesha mapendo, kama Yohana yule mwanafunzi ambaye alipendwa na Yesu na alisimama chini ya msalaba wake naye akamkabidhi mama yake Bikira Maria.

“Pamoja na mambo mengine, kwa namna ya pekee niliposimama chini ya msalaba alinikabidhi mama yake, nilikuwa mtoto katika familia yake. Kwa nini niseme mimi kama Yohana yule mwanafunzi aliyependwa na Yesu kutokana na mambo makuu haya aliyonitendea,” alisema.

Alibainisha kuwa, alikuwa amekabiliwa na changamoto za maradhi ambayo hata hivyo, hakuyataja, katika kipindi cha mwaka mmoja lakini wasaidizi wake walifanya kazi kwa busara na hekima ya hali ya juu bila hata yeye kuwaelekeza lolote.

“Kutokuwepo kwangu katika kipindi cha mwaka mmoja, jimbo halikuteteleka, pamoja na sala zenu asante sana kwa moyo wenu wa kujitoa.

“Kwa kadri Mwenyezi Mungu atakavyonipa nguvu na uwezo wa kufanya kazi katika kipindi changu cha ujana wa miaka 70, nitaendelea kuwatumikia, kwa njia ya sala na maombi nitakuwa pamoja nanyi kwa nguvu zaidi, Mwenyezi Mungu atujalie sote miaka mingi kwa kadiri ya mpango wake.

“Kabla Mungu hajanichukua ningependa Jimbo la Dar es Salaam liwe limetimiza parokia 100,” alisema.

Aidha, Mwadhama Pengo aliwashukuru mapadri wote na watawa wa jimbo hilo kuwa, walionesha ushirikiano mzuri na wasaidizi wake na hivyo jimbo hilo kuendelea vizuri.

Hata hivyo, baada ya kumaliza ibada hiyo ya misa takatifu kulifanyika hafla fupi ya kumpongeza iliyohudhuriwa na wasaidizi wake, mapadri, watawa wa kiume kwa wake pamoja na wawakilishi kutoka jumuia mbalimbali katika jimbo hilo.

Awali, Askofu Msaidizi Mdoe katika mahubiri yake, alisema Mwadhama Pengo aliyetimiza miaka 70 Agosti 5, mwaka huu, siku hiyo alikuwa nchini India katika matibabu.

Alisema katika nchi hiyo, alikwenda zaidi ya mara ya tatu kupata matibabu na huko Ujerumani nako mara moja.

Hata hivyo, alisema kwa neema ya Mungu anaendelea vizuri huku akifurahia miaka 43 ya upadri, 30 ya uaskofu na miaka 16 ya uaskofu mkuu.

Aidha, Mdoe alisema katika kipindi hicho aliitumia vema talanta aliyopewa na Mungu kwa kufanya mambo mazuri ya mfano nchini na hata nchi za nje.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo