Watuhumiwa wengine watatu wamefikishwa kwenye Mahakama ya Wilaya
ya Kiteto mkoani Manyara, wakituhumiwa kwa mauaji ya wakulima saba
yaliyotokea kwenye kata za Matui na kufikisha idadi ya watuhumiwa 16.
Awali, kulikuwa na watuhumiwa 13 waliofikishwa
mahakamani hapo ila juzi waliongezwa watatu kwenye kesi hiyo ambao ni
Leitinga Simon (26) na Lekomoi Pati (20) wote wakazi wa Kijiji cha
Ngeroni na Popo Lemnae (23) mkazi wa Matui.
Ilidaiwa mahakamani hapo mjini Kibaya na mwendesha
mashtaka Mbaruku Mohamed, mbele ya hakimu Majidi Hudi, kuwa washtakiwa
hao walitenda kosa hilo kati ya Novemba 11 na 12, mwaka huu.
Hata hivyo, washtakiwa hao hawakutakiwa kujibu
chochote kwenye mashtaka hayo kwani mahakama hiyo haina uwezo wa
kusikiliza shauri hilo na Hakimu Hudi aliahirisha kesi hiyo hadi Januari
30 itakapotajwa tena.
Kwenye kesi hiyo watu wanne kati yao wameshtakiwa
kwa mauaji pekee na watu tisa wameshtakiwa kwa mauaji hayo na pia
kudaiwa kuiba mifugo ambayo ni ng’ombe 309 zenye thamani ya Sh213
milioni mali za wafugaji wa Kijiji cha Matui.
Mohamed aliwataja washtakiwa hao wanne waliohusika
na mauaji kuwa ni Kirundi Sisini (45), Lazaro Pastei (30) na Yokoyeti
Koroboi (20) wote wakazi wa Kijiji cha Ilela na Kimai Enongoi (35) mkazi
wa Kijiji cha Namelock, wilayani Kiteto.
Aliwataja walio na kesi ya mauaji na kuiba mifugo
309 ni Seif Juma (40), Mohamed Ahamad (18), Shaabani Mkoloni (21), Said
Hatibu (29), Nasoro Hassan (25), Ayub Musa (18) Lucy Yohana (30) Abasi
Mohamed (25) wote wakazi wa Dosidosi na Mashaka Chibaleu (27) mkazi wa
Kijiji cha Engusero.
Alisema washtakiwa hao wanadaiwa kuwaua Hassan
Kundajo (62), Salum Iddi Juma (70) Lematui Sendalo (46), Julius
Andrew(50), John Makavu (42), Juma Omari Bakari (65) na Maria Ole
Siriana (36).