Mkurugenzi wa ufundi wa klabu bingwa Tanzania bara Azam FC, Sadi
Kawemba amesema walikua hawana mpango wowote na mshambuliaji kutoka
nchini Burundi, Amis Tambwe ambae amejiunga na Dar es salaam young
Africans baada ya kutemwa na klabu ya Simba katika dirisha dogo la
usajili.
Kawemba amesema taarifa za Azam FC kumuhitaji Amis Tambwe zilikua
zinavumishwa na vyombo vya habari lakini hawakuwahi kuonyesha hata
dalili za kumsajili mshambuliaji huyo ambaye alimaliza msimu uliopita
kwa kuibuka kinara wa upachikaji mabao kwenye ligi kuu ya soka Tanzania
bara.
Amesema kikosi chao kina wachezaji wa kutosha katika safu ya
ushambuliaji na katika mapendekezo waliyoyapokea kutoka kwa kocha wao
Joseph Marius Omog kupitia ripoti aliyoiwasilisha kwa viongozi mara
baada ya kucheza michezo saba ya ligi kuu ya soka Tanzania bara kulikua
hakuna ombi la kuongezwa kwa mshambuliaji.
“Tupo vizuri tunae Kavumbagu, nahodha wetu John Bocco anarudi hivi
karibuni uwanjani, tuna Gaudence Mwaikimba, Kipre Tcheche, Khamis Mcha
na bado kuna wachezaji ambao wana uwezo wa kucheza wakitokea pembeni na
kusaidia mashambulizi hivyo hatuoni sababu ya kuongeza mchezaji
mwingine.”
“Tabwe alikua anapendekezwa na watu tumsajili hususan mashabiki
lakini tuliona hakuna nafasi ya kufanya hivyo kutokana na kuamini wapo
wachezaji ambao wana uwezo wa kutusaidia katika michuano ya ligi kuu
pamoja na ile ya klabu bingwa Afrika.” Amesema Kawemba.
Katika kipindi cha dirisha dogo la usajilia mbacho kilifungwa rasmi
mwanzoni mwa juma hili Azam FC imewasajili Pascal Wawa, Majwega na Amri
Kiemba huku iliowaacha ni Ismail Diara raia wa Mali pamoja na Mhaiti
Lionel Saint-Preux