SHAHIDI WA KESI YA RUSHWA INAYOMKABILI HAKIMU AFARIKI DUNIA

UPANDE wa mashitaka kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), wameithibitishia Mahakama ya Wilaya ya Ilala kwamba aliyetakiwa kuwa shahidi wa pili katika kesi ya rushwa ya Sh 50,000 inayomkabili Hakimu Grace Kivegele na Karani wake, Rose Kuhima wa Mahakama ya Mwanzo Buruguri, amefariki dunia.

Katika shauri lililopita Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Devota Mihayo alidai mahakamani hapo kuwa aliyekuwa shahidi wa pili katika kesi hiyo, Cresencia Mruma amefariki dunia, lakini aliomba kuthibitisha kifo hicho.

Hata hivyo, jana upande huo wa mashitaka ulikuwa na shahidi Rehema Makson (45) ambaye alidai kwamba Aprili 22, mwaka huu, alipigiwa simu kutoka Kituo cha Polisi cha Tabata waliomueleza kwamba mtoto wake amekamatwa na kwamba siku hiyo alipelekwa mahakamani.

Makson alidai siku hiyo alishindwa kwenda kituoni kwa kuwa alikuwa safarini na kwamba Aprili 23, mwaka huu, alifika kituoni hapo na kuelezwa kuwa mwanawe amepelekwa mahakamani na kwamba alikuwa katika Gereza la Segerea.

Alidai polisi wa kituo hicho walimpa namba ya kesi ambayo ni kesi namba 471/2014 pamoja na jina la Hakimu; na kwamba siku hiyo hiyo alifika mahakamani na kuomba utaratibu wa dhamana kwa mshitakiwa.

Akiongozwa na Mihayo, shahidi huyo alidai alimuomba karani wa Mahakama ya Mwanzo Buguruni amuelekeze jinsi ya kumpatia dhamana mtoto wake.

Alidai kwamba alitakiwa kuwa na wadhamini wawili na barua mbili zenye picha kutoka katika serikali za mitaa.

Makson alidai Mei 5, mwaka huu, alifika mahakamani hapo kwa kuwa ndiyo siku ya mshitakiwa kufikishwa mahakamani kusomewa mashitaka yake, baada ya kesi kuitwa Hakimu Kivegele alimuuliza kama alikuwa na Sh 50,000 naye alimwambia kuwa hana.

‘’Kwa sababu tulitakiwa kuwa wadhamini wawili, tulishaurina na ndugu yangu Mruma (sasa ni marehemu) kwamba twende Takukuru tukapate msaada kuhusu tukio la kuombwa Sh 50,000 bila ya kusoma barua tulizokuwa nazo,’’ alidai Makson.

Aliendelea kudai kwamba walipofika katika Ofisi za Takukuru, Ilala, waliambiwa warudi mahakamani na wamuoneshe barua hizo Hakimu Kivelege na baadaye waliporudi, Mruma alimuonesha barua hizo Hakimu Kivelege, lakini aliwauliza kama walikuja wakiwa kamili kwa maana ya kuwa na fedha walizohitaji.

‘’Kwa mara nyingine, tulirudi tena Takukuru nao walituambia turudi mahakamani hapo siku inayofuata ambapo Ofisa kutoka taasisi hiyo alimkabidhi Mruma Sh 50,000 ndipo tulienda mahakamani huku tukiwa na ofisa huyo na kumkuta Hakimu Kivelege akiwa na kesi nyingine za kusikiliza,’’ alidai.

Shahidi huyo alidai Mruma alionana na Kivelege na kwamba alielekezwa kuwa fedha hizo ampatie askari; lakini kutokana na kwamba fedha hizo zilitoka Takukuru hawakuweza kumkabidhi mtu mwingine.

By Francisca Emmanuel 


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo