MTUMISHI WA HOSPITALI YA WILAYA YA GEITA AKAMATWA AKITOROSHA DAWA ZA WAGONJWA

Walinzi wawili wamemkamata mtumishi wa Hospitali ya Wilaya ya Geita, kwa kile kinachodaiwa kuwa alikuwa akitorosha dawa alizochukua katika wodi za wagonjwa.
 
Walinzi hao wa kampuni ya ulinzi ya GSG walimkamata mtumishi huyo juzi saa 1:00 asubuhi, kwenye lango kuu la hospitali hiyo alipokuwa akitoka kwenda nyumbani kwake.
Kaimu mganga mfawidhi wa hospitali hiyo, George Rweyemera alisema uongozi wa hospitali unaendelea kuchunguza kujua jinsi alivyozipata dawa hizo kwa kuwa hahusiki katika kitengo cha dawa.
“Nimeona mnaongea na walinzi pale. Hao wapo chini ya hospitali. Tunaendelea na uchunguzi kujua huo mzigo ameupataje, yule mama hahusiki na dawa,” alisema Rweyemera.
“Tukikurupuka tutakosa mengi, kwa hiyo nyie tulieni nitawapa taarifa sahihi zilizokamilika,” aliongeza.
Mfamasia wa hospitali hiyo, Dk Charles Alfred alikiri mtumishi huyo kukamatwa na kwamba dawa hizo alizichukua kwenye wodi.
Dk Alfred alisema kuwa mtumishi huyo aliiba dawa 21 za watoto, mirija 25 ya chupa za maji, cannular 50 za kushikia dripu za dawa, sindano 100 na chupa 10 za dripu zenye ujazo wa milita 500, zote zina thamani zaidi ya Sh100,000.
Mlinzi wa kampuni hiyo, Sadick Maganga alisema juzi saa 1:00 asubuhi alimtilia shaka mama huyo wakati alipokuwa akipita kwenye lango hilo.
Alisema alikuwa na kikapu alichokitoa nje, kisha akarudi hospitalini akidai kuna kitu amekisahau.
“Aliporudi ili atoke nje ndipo nikamtilia shaka, nikatoa taarifa kwa msimamizi wangu. Tulipokwenda kuangalia kikapu kile tukakuta kuna dawa,” alisema Maganga.

Na Salum Maige, Mwananchi


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo