KUTOKA NJOMBE: KATIBA MPYA HAIWEZI KUWA NA FAIDA BILA WANANCHI KUELIMISHWA

NA KENNETH NGELESI,EDDY BLOG NJOMBE

ASKOFU Mkuu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Jackobo Chimeledya, amesema katiba haitakuwa na faida kwa watanzania, iwapo  wananchi hawataelimishwa na kupewa muda wa kutosha kabla ya kupiga kura ya maoni.

Rai hiyo ilitolewa hivi karibuni  na Askofu huyo  mkoani hapa, wakati wa ibada ya  kumuweka Wakfu Askofu Mathew Mhagama, kuwa Askofu wa Nane wa Jimbo la Kusini Magharibi Tanganyika ,katika kanisa  kuu la Mtakatifu Andrea Mjini Njombe.

Alisema kuwa kwa kuwa katiba hii  haiwezi kutumika kwenye uchaguzi mkuu  ujao alishauri kuwa na  muda mrefu wa kutoa elimu kwa wananchi kabla ya kuanza zoezi la kura ya maoni ili, kila mmoja  awe na uelewa wa kupiga kura ya ndiyo ama hapana.

“ Ingekuwa ni amri yangu ningependa wananchi wapewe elimu ya kutosha hata ikibidi kuanzia miaka miwili hadi mitatu, ili wajue na wawe na ufahamu wa kutosha, na hiyo itasaidia kufanya maamuzi sahihi yakura ya ndio ama hapana  ya katiba.

Aidha  Askofu Chimeledya pia aliwataka viongozi wote wakiwemo wa dini,serikali na siasa kuheshimu mawazo ya wananchi, na kuwataka viongozi kuzingatia maadili, na kudai  kuwa ikiwa kipengele cha maadili ya  viongozi kitaondolewa kwenye katiba, kutakuwa na mapungufu mengi kwenye utendajikazi.

“ Katiba ni msingi wa kuleta maisha bora kwa kila mtanzania ni bora kama kunavitu vya kubadili,vibadilike kwamanufaa ya wananchi na taifa kwa ujumla hata kama ni miaka mitano ili mradi tuwe na kitu kizuri” Alisema Askofu huyo.

Naye Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu, aliyekuwa mgeni rasmi kwenye ibada hiyo, akimuwakilisha waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mizengo  Pinda ,alisema jamuhuri itaendelea kuheshimu uhuru wa kuabudu.

Waziri Nyalandu aliwahakikishia viongozi wa dini kuwa serikali ya Jamuhuri ya Muungano itaendelea kutoa uhuru wa kuabudu kwa dini zote huku akiwataka viongozi wa dini kuhakikisha wanawasaidia vijana ambao ni taifa la kesho kwa kuwalea kwenye maadili.

Hata hivyo serikali iliahidi kuchangia shilingi milioni 50 kwenye mradi wa kupanda miti kwaajili ya utuzaji wa mazingira,huku waziri huyo na familia yake wakiahidi shilingi milioni kumi kwaajili ya kusaidia mfuko wa Akofu wa Jimbo hilo wa kusomesha watoto Yatima.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo