WAZIRI wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza, nusura atokwe na machozi baada ya kukuta bwawa la umwagiliaji lililojengwa kwa zaidi ya sh. bilioni 3 limebomoka.
Hali hiyo ilimfanya awaweke kitimoto wahandisi wa Ofisi ya Umwagiliaji Kanda ya Mbeya.
Alisema
ujenzi wa bwawa hilo ambalo lilikuwa linatarajiwa kutumiwa na wananchi
zaidi 6,000 umejaa harufu ya ufisadi, hivyo ataunda tume itakayochunguza
zabuni ilivyotangazwa,uwezo wa mkandarasi, matumizi ya fedha na
utaalamu uliotumika.
Alisema
hatua hiyo inalenga kuhakikisha kila aliyehusika kutoka katika wizara
yake, Ofisi ya Umwagiliaji Kanda ya Mbeya hasa wasimamizi ili
kuhakikisha wanawajibishwa.
"Hapa
tunazungumza habari za utaalamu nami kama mhandisi mwenzenu nawaambieni
wazi kuwa hapa mmeniangusha na kunifedhehesha,kwani mmenipa wasiwasi
mkubwa jinsi mlivyoteketeza mabilioni ya fedha za kodi za Watanzania
ambayo yangetumika kuwasaidia wengi, sasa nasema nataka kupata taarifa
kamili baada ya uchunguzi," alisema.
Alisema
kuwa wakati zaidi ya bilioni tatu zimetumika bila mradi kukamilika
anashangaa kusikia kuwa mkandarasi wa kampuni ya Boymanda iliyojenga
wigo huo ikidai kuongezewa zaidi ya milioni 600 kwa ajili ya kumalizia
kazi hiyo jambo ambalo ni wizi mkubwa wa fedha za Watanzania.
Chiza
alisema amekerwa na majibu ya wahandisi wake na ushirikiano uliokuwepo
na wahandisi wa Halmashauri ya Mbarali. Alisema kazi ya Serikali lazima
ifanywe kwa ushirikiano mkubwa bila ya kuwa na kificho.
