DIWANI WA CHADEMA AWA MFANO WA KUIGWA, KATA YAKE YAIBUKA KIDEDEA UJENZI WA MAABARA

MKUU wa mkoa wa Singida, Dk Parseko Kone amemmwagia sifa tele diwani wa kata ya Mwangeza, katika halmashauri ya Mkalama mkoani Singida, Petro Mliga (CHADEMA) kwa kuwezesha kata yake kuibuka ya kwanza kukamilisha ujenzi wa maabara.

Dk Kone alitoa kauli hiyo katika mji mdogo wa Iguguno wilayani Mkalama wakati wa kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku nne kukagua maendeleo ya ujenzi wa maabara shule za sekondari katika halmashauri za Mkalama na Iramba.

Alisema kuwa pamoja na diwani Mliga kuwa chama cha upinzani, ameweza kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kiwango cha hali ya juu na kwa muda muafaka.

Akionesha kufurahishwa na kazi nzuri aliyoifanya diwani huyo wa CHADEMA, Dk Kone aliwataka madiwani wengine waende kata ya Mwangeza kujifunza huku akisema kuwa mara alipokagua maabara hizo alilazimika kumwomba diwani huyo arudi CCM.

“Nilimwambia kwa nini usirudi nyumbani lakini yeye akanijibu kwani kuna shida gani kama natekeleza sera za CCM,” Dk Kone alikiambia kikao hicho cha majumuisho.

Mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa watu wa aina hiyo ndio viongozi wanaotakiwa kwa kuwa mapambano yao huishia jukwaani tu lakini wakishateremka jukwaani huchapa kazi kama kawaida.

“Hawa ni watu wanaogombea upinzani kwa nia ya kuwaletea wananchi wao maendeleo. Huyu ambaye sera yao ni kupinga kuchangia anawapita nyie wenye sera?” Dk Kone alihoji na kuwapa changamoto madiwani wa CCM .


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo