MTOTO
wa Rais Jakaya Kikwete, Ridhiwan Kikwete, amesema mzee wake (Kikwete)
hana ugomvi wala uhusiano mbaya na aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward
Lowassa; na kwamba kama kungekuwa na ugomvi, basi yeye angekuwa anajua
hilo.
Ridhiwan
alitoa kauli hiyo jana wakati akihojiwa na Televisheni ya Star TV
kupitia kipindi chake cha Changamoto za Kisiasa kwa Watoto wa Viongozi. “Wanaosema
uhusiano wa mzee (Rais Kikwete) na Lowassa ni mbaya ni waongo, si
mbaya... tatizo baadhi ya Watanzania wana tabia ya kupika vitu ili
wafanikiwe,” alisema Ridhiwan na kusisitiza;
“Sijawahi
kumwona mzee akiwa na ugomvi na huyu bwana (Lowassa) na hili lazima
nilisema, mimi nimeenda Ikulu zaidi ya mara tatu na kumkuta mzee (Rais
Kikwete) akiwa na Lowassa.”
Alisema baba yake hapendi ugomvi na wala hapendelei kuingia kwenye ugomvi na mtu.
Alipoulizwa
na mwongozaji wa kipindi kuwa kuna taarifa za kuvutana kisiasa kati ya
Rais Kikwete na Lowassa na kwamba kuna wakati upande wa Rais Kikwete,
umekuwa ukivutana na upande wa Lowassa kisiasa na wa Lowassa kuibuka
mshindi, Ridhiwan alisema;
“Hakuna siasa za kuvutana kati ya mzee na Lowassa, bali wanaosema hivyo wanataka kutengeneza mpasuko,” alisema na kusisitiza kuwa Rais Kikwete hana ugomvi na Lowassa.
Alisema; “Rais Kikwete ana vyombo vyote..nyie mnaona marais wengine wanayofanya... kama angekuwa na jambo na Edward mimi ningejua.” Alisema tatizo lipo kwenye media hawataki kueleza ukweli...hawataki kuweka vitu ambavyo watu wangependa kusikia.
Alipoulizwa
kuhusu kinyang’anyiro cha urais ni mtu gani yeye anamuona anafaa
kuwania nafasi hiyo, Ridhiwan alisema CCM ina watu wengi wanaofaa kuwa
viongozi, akitaja hawawezi kuwamaliza hivyo wale ambao hatawataja
atakuwa hajawatendea haki.
“CCM
ina watu wengi sana nikitaja wengine sitawatendea haki kwa kutowataja,
wapo wengine wenye sifa waliopo nje tutaangalia kati ya hao nani mwenye
sifa ya kupeperusha bendera yetu,” alisema Ridhiwan na kutolea mfano
mwaka 2005 akisema kati ya wagombea watatu waliokuwa wamebaki, ungesema
nani anafaa angekuwa Salim Ahamed Salim.
Wagombea
hao alikuwa Salim Ahamed Salim, Profesa Mark Mwandosya na Rais Jakaya
Kikwete. Alisema Salim alikuwa na uzoefu wa uongozi kimtandao na ndani
ya nchi, huku Profesa Mwandosya akiwa msomi mzuri na Rais akiwa na
uzoefu wa uongozi Serikalini na ndani ya chama.
“Lakini
Mzee Mkapa (Benjamin) hakuwa na uwezo wa kuwachagulia wanachama mtu
anayemtaka, wanachama waliamua wenyewe na kumpitisha Rais Kikwete, hivyo
ndivyo ilivyo kwenye chama chetu,” alisema.
Alipoulizwa ni kitu gani atakumbukwa nacho Rais Kikwete, endapo ataondoka madarakani; Ridhiwan, alisema; “Akiondoka madarakani Watanzania watamkumbuka kwa kuimarisha demokrasia...anastahili kupewa cheo cha baba wa demokrasia.”
Alisema asingekuwa mtu wa demokrasia angekuwa amefuta vyama vya siasa na hata kuwaondoa nchini baadhi ya watu.
“Watu wanakaa kwenye televisheni wanasema rais legelege, dhaifu...huwezi kumuita mzazi au baba wa mtu dhaifu, lakini tukimuuliza mzee huwa anajisikia vipi akiitwa hivyo, anasema huo ndio uongozi.”
“Watu wanakaa kwenye televisheni wanasema rais legelege, dhaifu...huwezi kumuita mzazi au baba wa mtu dhaifu, lakini tukimuuliza mzee huwa anajisikia vipi akiitwa hivyo, anasema huo ndio uongozi.”
Ridhiwan
alisema maendeleo si barabara peke yake, bali ni pamoja na kuwapa watu
uhuru wa kuzungumza. Ridhiwan alipoulizwa taarifa kwamba ana utajiri
kupindukia, alisema taarifa hizo si za kweli.
“Unaposema Ridhiwan ana majumba, basi yatajwe yapo wapi, sema nina nyumba ipo Dodoma karibu na CCM, lakini hawasemi.
"Unaposema ninamiliki vituo vya mafuta, basi vitaje sema ninamiliki Oil com,”
alisema na kuongeza kwamba yeye anamiliki nyumba moja jijini Dar es
Salaam ambayo alikuta imeanzishwa ujenzi na mzee wake (Rais Kikwete)
aliyompa wakati anataka kuoa.
Alisema hataki kujilimbikizia mali, maana akijilimbikizia mali hiyo haitakuwa sehemu ya mali za ndugu zake.