Waendesha pikipiki za kubeba abiria
maarufu kama boda boda, wamezitaka mamlaka za kisheria kuwachukulia
hatua kali watuhumiwa wanaobainika kujihusisha na wizi wa pikipiki,
ambao wamedaiwa kurudisha nyuma jitihada zao za kujikwamua na umaskini,
badala ya kuwakamata na kuwaachia,jambo linalowafanya wengi wao kuamua
kujichukulia sheria mikononi kwa kuwaadhibu.
Waendesha pikipiki hao wamesema hayo walipohojiwa kuhusiana
na wenzao kujichukulia sheria mikononi kwa kumpiga hadi kulazwa katika
hospitali ya rufaa ya mkoa wa Morogoro, mtuhumiwa Shafii Shomari,
aliyedaiwa kushirikiana na mwenzake kumpora pikipiki Saidi Omari,baada
ya kumkodi kutokea eneo la Itigi Msamvu, wakitaka kupelekwa eneo la
Mapumbani,kabla ya siku chache baadaye pikipiki hiyo kukutwa nje ya
nyumba ya mwenyekiti wa mtaa wa Mwembesongo,Nasoro Samata,aliyedai
kuachiwa pikipiki hiyo kama dhamana na mtu aliyechukua kwake mkopo wa
shilingi 50,000.
Akizungumzia tukio hilo la wizi wa pikipiki, kamanda wa polisi mkoa
wa Morogoro Leonard Paulo, amewashuruku raia wema waliofanikisha
kupatikana kwake baada ya kuibwa, na kwamba polisi wanaendelea na
uchunguzi zaidi wa tukio hilo ikiwemo kumhoji mwenyekiti huyo wa mtaa na
kuchunguza namna alivyoipata pikipiki hiyo
>>>itv
