KAMANDA WA POLISI AZUNGUMZIA TUKIO LA BASI LA MAGEREZA KUSHAMBULIWA KWA RISASI NA WANAOHISIWA KUWA MAJAMBAZI

Basi la Magereza lililokuwa limebeba wafungwa/maabusu limeshambuliwa kwa risasi na watu wanaosadikika kuwa ni majambazi leo (July 2) katika eneo la Mikocheni, Dar es Salaam.

Akizungumza, Kamanda wa polisi Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Camellius Wambura amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa jeshi la polisi limeanza kufanya uchunguzi.

Kamanda Wambura amesema ni mapema kutaja nia ya watu hao wenye silaha waliovamia gari hilo kwa kuwa wanaweza kuwa na nia tofauti kabisa na fikra za haraka.

“Tunafanya uchunguzi ambao utatufikisha mahali tuweze kubaini ni nini. Inawezekana pengine kuna wahalifu walikuwa katika harakati za uhalifu ghafla wakaona basi lile ambalo lina askari wazuri wenye silaha wakaanza kulishambulia…inawezekana. Au inawezekana vingine vyovyote ambavyo hatuwezi kufikiri wala kubaini.” Kamanda Wambura

Ameeleza kuwa hakuna maabusu yoyote aliyeweza kutoroka katika tukio hilo na kwamba madhara yaliyotokea kwenye gari hilo sio makubwa. Amesema bado hajapata taarifa yoyote ya uharibifu wa mali au upotevu wa mali uliotokea katika eneo hilo kufuatia tukio hilo.

Akizungumzia watu waliojeruhiwa katika tukio hilo, Kamanda Wambura amewataja watatu waliopata majeraha kuwa ni dereva wa basi hilo, mahabusu mmoja na askari mmoja wa kike.

“Kuna baadhi wana michubuko, wale wawili ambao ni dereva na mahabusu mmoja. Lakini kuna askari wa kike ambaye yeye ana majeraha kwenye kifua upande wa kulia. Lakini ni nini kimesababishia michubuko ile hatuwezi kujua kama ni vioo ama ni purukushanai wamejichubua mle ndani au vitu gani.” Amefafanua.

Kwa undani wa habari hii, usikose kusikiliza taarifa ya habari ya 100.5 Times Fm leo Moja na dakika 45 usiku, na pia katika kipindi cha The Jump Off kinachoanza saa mbili kamili hadi saa nne kamili usiku.

CHANZO: TIMES FM


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo