WALIMU SASA WATANGAZIWA NEEMA YA KUWA NA MWAJIRI MMOJA PEKEE

CHAMA cha Walimu Nchini (CWT), kimeipongeza serikali kwa kukubaliana na hoja yao ya kuwa na mwajiri mmoja.

Akizungumza na waandishi wa habari, Rais wa chama hicho, Gratian Mukoba, alisema CWT imefurahishwa na serikali kukubali kuunda chombo kimoja cha kuwaajiri walimu nchini.

Alisema CWT ilianza kudai uwepo wa mwajiri mmoja kwa walimu tangu serikali ya awamu ya tatu ili iwe rahisi kutatua kero za walimu nchini.

“Rais Benjamin Mkapa alisema angemwachia Rais wa awamu ya nne akisema kuwa jambo hili linahitaji mabadiliko ya sera na sheria…Rais Jakaya Kikwete alipoingia madarakani tunaamini alikabidhiwa jambo hili ambalo tumekuwa tukilipigania kwa miaka kumi,” alisema Mukoba.

Mukoba alisema walimu nchini ni asilimia 64 ya watumishi wote wa umma hivyo walihitaji chombo chao kimoja kitakachosimamia ajira yao kama njia ya kumaliza migogoro ya mara kwa mara.

Alisema kwa kuwa azimio la Bunge limepitishwa , CWT inaishauri serikali isijifungie ndani peke yake na kutoa chombo hicho bila kuwashirikisha walimu.

“Tunachelea kisijekuwa chombo chenye majukumu yasiyokidhi na kusanifu shida za ajira ya walimu ikiwemo usafiri, mishahara na kiinua mgongo,” alisema Mukoba.

Aidha, alisema hatua ya kutawanya majukumu ya walimu katika mamlaka mbalimbali kimesababisha kwa kipindi kirefu walimu kuishi na kero zisizopatiwa ufumbuzi wa kudumu.

Alisema kwa kuwa maandalizi ya katiba mpya yanafanyika CWT inashauri chombo hicho kiwekwe kwenye Katiba mpya kama ilivyo kwa Kenya ambapo chombo hicho kinafanya kazi vizuri.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo