MWILI WA KIKONGWE ALIYEUAWA WAKUTWA PORINI UKIWA UMELIWA NA FISI WILAYANI KAHAMA

Kifo cha Mkazi wa kitongoji cha Ikandilo kata ya Mwendakulima wilayani Kahama Mkoani Shinyanga Butamo Maziku (80) aliyedaiwa kuuawa na Fisi usiku wa kuamkia jana, kimechukua sura mpya baada ya kubainika ni uongozi umedanganya umma. 


Siri hiyo imefichuka jana baada ya Jeshi la Polisi wilayani humo kufika kwenye tukio na kuthibitishiwa kwamba Marehemu Maziku aliuawa na watu akiwa nyumbani kwake na kutupwa kwenye vichaka ili ijulikane kuwa ameuawa na Fisi. 



Juma Kabado mjukuu wa Marehemu Butamo aliyehojiwa na kuachiwa huru amekaririwa akiuambia umma kwamba, katibu wa Sungusungu wa sehemu hiyo Athumani Kisaka aliwaelekeza watu waseme Butamo ameuawa na Fisi vinginevyo wangeweza kusumbuliwa. 

Imeelezwa, baada ya maelekezo hayo, Kisaka pia aliwaambia ndugu na majirani waseme marehemu Maziku alikuwa akiishi bila ndugu kijijini hapo wakati anao wajukuu wawili; Juma Kabado na dada yake aliyetambulika kwa jina la Regina aliyedaiwa kutoroka. 

Jamii imegubikwa na mashaka kufuatia madai kwamba Marehemu Butamo aliuaawa usiku wa kuamkia jana, wakati damu iliyokutwa nyumbani kwake imeonesha kuwa ina siku nyingi, na mwili wake umekutwa umeharibika vibaya vichakani humo. 
Watu saba wameshikiliwa na Jeshi la polisi kufuatia upotoshaji wa taarifa hizo akiwemo Fredrick John (Mme wa Rebeka ambaye ni Mjukuu wa Butamo), na Athumani Kisaka (Katibu wa Sungusungu), anayedaiwa kusingizia Butamo kuuawa na Fisi. 
Wengine wanaoshikiliwa na Jeshi hilo ni, Shaaban Juma, Jummanne Ally, Hamis Rashid, Mayala Maganga na Luhumbika Lubigili, wote wakazi wa kijiji hicho na ndiyo walioshiriki katika kutoa taarifa za uongo kwa Jeshi la Polisi. 

Na Marco Mipawa-Kahama


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo