CHADEMA WADAI WANAOPITA NA MABANGO KUWATAKA VIONGOZI WAKUU WAJIUZULU NI "MAMLUKI"

WAJUMBE wa Baraza Kuu la Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mkoa wa Pwani, wamelikana kundi la watu waliojitokeza hivi karibuni wakijiita viongozi wa chama hicho na kufanya mikutano yenye lengo la kukichafua na kuwataka viongozi wa kitaifa wajiuzulu.

Kwa niaba ya wenzake, Mwenyekiti wa CHADEMA Mkoa wa Pwani, Said Ukwezi, alisema kuwa wamelazimika kutoa tamko hilo baada ya kubaini kwamba wanaofanya mikutano hiyo na vyombo vya habari si wanachama wa chama hicho.

Ukwezi alisema kuwa hivi karibuni kumezuka mtindo wa kukichafua chama hicho, ambao unaratibiwa na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa mgongo wa waliokua viongozi wa CHADEMA wakafukuzwa na kutimkia ACT-Tanzania.

Alisema kuwa kundi hilo limewahadaa Watanzania kwa kujitambulisha kuwa ni viongozi wa CHADEMA, huku wakiwa mstari wa mbele kushiriki bila kificho kazi na majukumu ya ACT-Tanzania, kama kugawa kadi na kushawishi watu kuhama CHADEMA.

“Mtakumbuka Juni 23 mwaka huu, kundi hilo liliitisha mkutano na waandishi wa habari katika Hoteli ya Lamada jijini Dar es Salaam na kwa kiasi kikubwa mkutano huo uliitishwa kwa lengo la kuchafua hali ya hewa na kujaribu kuwaaminisha Watanzania kuwa hali ya CHADEMA ni tete, lakini ukweli wa mambo ni kuwa hali ya chama chetu ni shwari,” alisema.

Kwa mujibu wa Ukwezi, wanakosa majibu sahihi kuhusu ajenda ya kundi hilo kwani katika kipindi hiki chama hicho kipo katika uchaguzi ngazi ya kata na Septemba watakamilisha ngazi ya taifa, hivyo kama kundi hilo limeona viongozi hao hawafai lingesubiri wakati wa uchaguzi mkuu badala ya kukimbilia kutoa matamko yasiyo na tija.

Katika tamko lao, wajumbe hao wameeleza kuridhishwa na viongozi wa kitaifa waliopo madarakani kutokana na kuongeza idadi ya wanachama kuanzia ngazi ya vitongoji, mitaa, kata, wilaya hadi mikoa.

Kwamba kupitia viongozi hao wa kitaifa, programu ya CHADEMA ya msingi imefanikiwa kukipeleka chama kuwa mtandao mkubwa na kuweza kukabiliana na hila za CCM.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo