HAKIMU WA WILAYA YA KARAGWE AAMUA KUACHA KAZI GHAFLA, AGOMA KUTAJA SABABU

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, Hakimu wa Wilaya ya Karagwe, mkoani Kagera, Peter Matete, ameacha kazi ghafla, huku akikwepa kutaja sababu ya hatua hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana  mjini Kayanga, hakimu huyo alisema kuwa ameamua kuacha kazi na tayari amemwandikia barua Jaji Mkuu tangu Aprili 23 na kutoa saa 24 za kuacha kazi.

Matete alidai kuwa amesalimisha mshahara wake wa mwezi mmoja, huku akisisitiza kutosema kile kilichomsukuma kuchukua hatua hiyo isiyokuwa ya kawaida.

“Sitaki msumbuke kujua sababu zilizonifanya kuacha kazi. Sina shinikizo lololote, mimi ni mtu mzima na nina akili timamu, mnalopaswa kuelewa nimeacha kazi,” alisema Matete.

Wakati akichukua hatua hiyo, mahakama za Wilaya ya Karagwe katika kipindi cha kuanzia Januari mwaka huu zimekuwa zikilalamikiwa na wananchi, vyama vya siasa na asasi za kiraia kwa kuongezeka kwa vitendo vya rushwa na ukiukwaji wa haki za binadamu.

Katika kilele cha shutuma hizo, Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Karagwe, Benson  Bagonza,  Februari 11, mwaka huu aliitisha maandamano ya wachungaji 80 ya kupinga  na kulaani vitendo vya rushwa vinavyoendeshwa katika mahakama mbalimbali zilizopo Wilaya ya Karagwe.

Alisema  wananchi hasa wasiokuwa na kipato wamekuwa wakinyanyaswa  kwa kunyimwa dhamana  na kutakiwa kutoa  kiasi cha shilingi laki tano  ili kuweza kupewa dhamana, huku wengine wakipelekwa rumande bila hatia.

Hata hivyo  kiongozi huyo wa kiroho alisema vyombo vya dini vilikuwa vikichukiwa na mamlaka mbalimbali za juu  kutokana na kusikika vikilaani rushwa, ufisadi na wananchi  kunyimwa haki zao za kikatiba.

 NA Mbeki Mbeki,Kagera


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo