MKUU WA WILAYA YA MAKETE ATEMBELEA ENEO LILILOKUMBWA NA MAAFA KIJIJI CHA NDULAMO

Mkuu wa wilaya ya Makete Mh Josephine Matiro amefanya ziara kwenye eneo la Kitongoji cha kwa Yuta, kijiji cha Ndulamo kata ya Iwawa wilayani hapo ambacho kimekumbwa na maafa ya nyumba kuezuliwa na upepo mkali jana majira ya saa 11 jioni

Mkuu huyo wa wilaya ambaye ameambatana na kamati ya ulinzi na usalama wilaya kwa kushirikiana na viongozi mbalimbali wa halmashauri ya wilaya ya Makete, wamesikitishwa na maafa hayo ambayo yameacha simanzi kubwa kwa wananchi hasa wamiliki wa nyumba hizo

Akizungumza na baadhi ya waathirika walioezuliwa nyumba zao Mh Matiro amewapa pole kwa janga hilo lililowakumba ambapo ameshuhudia mwenyewe hali ilivyokuwa ya baadhi ya nyumba kubomoka kuta zake, mapaa kusombwa pamoja na bati kupeperushwa mbali huku baadhi ya vipande vikionekana kunasa kwenye miti

Katika taarifa ya awali iliyotolewa kwa mkuu wa wilaya na Afisa Mtendaji wa kata ya Iwawa Bw. Festo Msigwa imesema kuwa jumla ya kaya nane zimepatwa na maafa hayo pamoja na jiko la shule ya msingi Ndulamo na kufanya jumla ya nyumba 11 kuathirika na janga hilo

Aidha mkuu wa wilaya ameagiza kijiji kufanya tahmini ya haraka ili ijulikane ni athari kiasi gani kimetokea akitolea mfano idadi ya bati na mali za wahanga hao kwa ujumla ili serikali ione namna ya kufanya haraka iwezekanavyo

Kwa upande wake mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Makete ambaye naye alikuwepo eneo la tukio amesema kesho Jumatatu asubuhi na mapema atatuma timu ya wataalamu kufika kwa ajili ya kufanya tathmini ili ijulikane ni kiasi gani cha maafa na hasara iliyotokea

Afisa mtendaji wa kijiji cha Ndulamo Bw. Majuto Mbwilo amesema kwa sasa uongozi wa kijiji umewaombea wahanga kwnye nyumba za jirani ambapo ndipo wanapoishi hadi sasa wakati taratibu nyingine zikiendelea

Miongoni mwa wahanga ambaye nyumba yake mbali na kuezuliwa pia imebomoka yote bw.Imma Mahenge amesema wakati tukio hilo linatokea hakuwepo nyumbani hivyo anamshukuru Mungu kwa kumnusuru lakini anaumia kwa kuwa nyumba yake yote imesambaratika

Tukio hilo limetokea jioni ya jana Februari 15 majira ya saa 11 jioni


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo