SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limesema changamoto kubwa
linaloikabili sasa ni madeni ya mamilioni ya fedha waliyoyarithi kutoka
uongozi uliopita wa Rais, Leodegar Tenga.
Akizungumza katika tathimini yake ya siku 100 tangu
alipochaguliwa kuwa rais mpya wa shirikisho hilo, Jamal Malinzi, alisema
madeni hayo ni makubwa ukilinganisha na kipato cha TFF kinachotegemea
zaidi mapato ya milangoni ya mechi mbalimbali.
“Madeni tuliyoyakuta ni makubwa, lakini mengine tumegundua ni hewa,
hivyo yanafanyiwa uhakiki ili tujue madeni halisi ili tuweze kuyalipa,”
alisema Malinzi aliyeingia madarakani Oktoba 27, mwaka jana.
“Pia tunafanya mazungumzo na watu wanaoidai TFF ili watupe masharti nafuu ya kulipa madeni hayo.”
Kauli ya Malinzi imekuja ikiwa imepita miezi sita tangu TFF ipate
aibu ya mabasi yake kukamatwa na Kampuni ya Udalali ya Flamingo ili
kufidia deni la zaidi ya Sh50 milioni.
