MGOGORO wa walimu wapatao 811 wa Halmashauri ya Ujiji mkoani
KIGOMA, umemalizika baada ya Halmashauri hiyo kuridhia na kuacha mara
moja kukata asilimia mbili za mishahara ya walimu hao kisha kupeleka
fedha hizo kwenye Chama cha walimu Tanzania(CWT).
Taarifa ya walimu hao kwa vyombo vya habari, iliyosainiwa na
Mwenyekiti wa walimu, K. Sabibi, imesema mgogoro huo ulidumu kwa miaka
miwili na nusu na tangu Octoba ,2013, Halmashauri hiyo imekubali
kusitisha makato hayo kwa waliokuwa wamejitosa kupigania haki zao.
‘’Shukrani kwa viongozi wote hasa mkuu wa wilaya ya Kigoma,
Ramadhan Maneno na wasaidizi wake, waliohakikisha mgogoro huo
unamalizika kwa amani’’ imesema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imemshukuru pia Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigoma
Eng.Boniface Nyambele kwa uelewa wake na kukubali kuchukua hatua za
makusudi kwa kusimamisha makato hayo kwenda CWT yaliyokuwa yakifanyika
kinyume cha sheria tangu mwaka 2011.
Wamesema makato hayo yalikuwa yakifanyika kinyume na sheria ya
ajira na mahusiano kazini kama kifungu cha 61(4) na 5 kinavyoeleza.
‘’Tunapenda ifahamike kwa walimu wenzetu na umma wa Watanzania kuwa
mgogoro uliokuwepo kati ya walimu wa Kigoma ujiji na mwajiri yaani
Mkurugenzi, umekwisha malizika’’
‘’Kwa kuwa mgogoro huo umekuwa wa muda mrefu na vyombo vya habari
vimekuwa vikitoa taarifa, tunavishukuru sana kwa kazi nzuri kwa
kuhabarisha walimu wenzetu na wananchi’’ imesema taarifa hiyo.
Imeeleza kuwa, kuwepo kwa mgogoro huo kuliathiri utendaji kazi wa walimu hao kwa namna nyingi ingawa si kwa kiwango kikubwa.
Sanjari na hayo, walimu hao wamevikumbusha vyama vya wafanyakazi na
waajiri, kufanya kazi kwa kufuata sheria za kazi siyo mazoea na kwamba
ikumbukwe kuwa kukata mshahara wa mwajiriwa bila ridhaa yake ni kosa
kama inavyofanya CWT kwa walimu kote nchini.