BAADHI
ya wanafunzi wa shule za msingi mkoani Pwani wenye virusi vya Ukimwi,
wamesema baadhi ya walimu huwataka kimapenzi licha ya kuwaeleza ukweli
juu ya hali zao kiafya.
Wametaka
Serikali na asasi za kiraia kusaidia kushughulikia walimu na wanajamii
wanaoshawishi watoto kwa ujumla kuingia kwenye uhusiano nao wa
kimapenzi.
Wamesema
changamoto hiyo, husababisha baadhi kupata tabu katika masomo yao hasa
katika suala la ufaulu, kutokana na kujikuta wakipunjwa alama kwa
makusudi wanapokataa kuingia uhusiano na walimu.
Hayo
yalielezwa kwenye semina ya wiki mbili kwa watoto wenye umri wa miaka
mitano hadi 14 wanaoishi na VVU, iliyoshirikisha pia walezi na wazazi
wao Kibaha mkoani Pwani.
“Mi
sijaanza kutumia dawa za kupunguza makali ya Ukimwi (ARV’s), lakini
najitambua kuwa naishi na virusi hivyo. Tatizo kubwa tunalokumbana nalo
sisi watoto na hata wale ambao hawana virusi ni vishawishi vya ngono kwa
watu wazima, kwa mfano mimi na rafiki yangu kuna walimu shuleni
walitutongoza, ukikataa anakuchapa fimbo,” alisema mmoja wa watoto.
Baadhi
ya watoto waliozungumza na mwandishi, walisema licha ya walimu, baadhi
ya watoto wamejikuta katika wakati mgumu kutokana na kushawishiwa
kimapenzi na jamaa bila kujali kuathirika kwao na virusi.
Walishukuru
shirika linalotoa huduma za kichungaji kwa watu wanaoishi na virusi vya
Ukimwi mkoani Pwani na Dar es Salaam chini ya Kanisa Katoliki Jimbo Kuu
la Dar es Salaam (Pasada) kwa msaada wa elimu ya namna ya kujikinga na
maambukizi mapya na kuishi kwa matumaini ili kutimiza ndoto zao kupitia
mradi wa “Kivuko na Watoto”.
Mkuu
wa Idara ya Elimu na Mafunzo wa Pasada, Nelson Chiziza alisema mradi wa
Kivuko kwa Watoto unalenga kuboresha mahusiano na mawasiliano kati ya
mzazi, mlezi na mtoto anayeishi na maambukizi ya virusi vya Ukimwi,
kuwajenga kimaadili, kujua namna ya kuboresha afya zao na matumizi
sahihi ya ARV’s.
Awali
akifunga semina hiyo iliyoshirikisha watoto 22 na walezi wao,
Mkurugenzi Mtendaji wa Pasada, Yohana Simon alisema mradi huo ulianza
kwa majaribio mwaka jana baada ya mchakato wa uanzishwaji wake kuanza
mwaka 2011 .
>>Habari leo
>>Habari leo
