Mratibu wa Harambee Meneja wa miradi wa kituo cha Moyo kwa Moyo, Renatus Mpiluka
akizungumza kuhusu harambee katika ofisi za kituo hicho mjini Iringa.
Consolata Sanga meneja wa fedha wa CPEC kushoto , Renatus Mpiluka
meneja mradi na Destory Wikedzi Mkurugenzi wa CPEC wakiwa katika picha
ya pamoja katika ofisi hizo (Picha zote na Denis Mlowe)
========= ========== ==========
WATOTO YATIMA KITUO CHA MOYO KWA MOYO KUFANYIWA HARAMBEE
Na Denis Mlowe,Iringa
SHIRIKA lisilo la kiserikali la Creating Partnerships to Empower
Communities (CPEC) la Iringa kwa kushirikiana na kituo cha radio cha Nuru Fm wameandaa
harambee ya kukichangia kituo cha watoto yatima cha Moyo kwa Moyo kilichoko
Matanana wilayani Mufindi.
Akizungumza na Tanzania Daima mratibu wa Harambee hiyo na
Meneja wa Miradi wa kituo hicho Renatus Mpiluka alisema lengo la harambee hiyo
ni kutunisha mfuko wa kituo hicho ili kuboresha huduma kwa yatima wapatao 300
wanaohudumiwa na kituo hicho.
Mpiluka alisema wameamua kufanya harambee hiyo kwa kuwa
waliokuwa wafadhili wa kituo hicho kutoka Sweden wamepunguza misaada zaidi ya
asilimia 70 kutokana na mtikisiko wa uchumi duniani.
Alisema watoto yatima wanamahitaji makubwa ya ada za shule
kwa wanafunzi wanaenda shule za sekondari, mavazi, chakula hivyo inawawia
vigumu kituo kumudu gharama za uendeshaji wa kituo hicho.
“Kituo kinakumbana na changamoto nyingi sana tangu wafadhili
kupunguza msaada hivyo tumeamua kufanya harambee ili tuweze kujiendesha na kuwasaidia
watoto hao yatima ambao kwa kweli ni wengi na ni jukumu letu kuweza kuwasaidia
kwa hali na mali katika kufanikisha ndoto zao za miasha” alisema Mpiluka
Mpiluka alisema changamoto hizo za mahitaji makubwa ya watoto
yatima zimepelekea kituo cha Moyo kwa Moyo kushirikisha wadau mbalimbali katika kuchangia
na kujitolea misaada mbalimbali kwa kituo hicho.
Alisema kituo kimefanikiwa kuwapatia mafunzo ya ufundi
watoto yatima na kuwawezesha kusoma masomo ya komputa na hivyo wafikishapo
miaka 18 waweze kujitegemea na kuwapatia huduma ya chakula watoto walioko
katika shule za msingi za Mufindi.
Katika harambee hiyo itakayofanyika siku ya Krismasi,Mgeni
rasmi anatarajia kuwa Mkurugenzi wa Tigo Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Jackson
Kiswaga na kusindikizwa na bendi ya Whispers
ya jijini Dar es salaam.
Kwa
yoyote anayetaka kuchangia katika harambee hiyo anaombwa atume kwa tigo
pesa 0655161678 na M-pesa 0756 56 56 03 au kwa kiingilio cha shilingi
20,000 kwa VIP na wakubwa 5000, watoto 2000. Kumbuka Kutoa ni moyo
usambe si utajiri