Kamanda
wa Jeshi la Polisi mkoa wa Singida, ACP. Geofrey Kamwela akitoa taarifa
kwa waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) juu ya kijana mmoja Saidi
Hamisi (34) kumbaka Kikongwe mwenye umri wa miaka 80 (jina
tunalo).Inadaiwa baada ya mtuhumiwa kumaliza kumbaka kikongwe huyo,
alilala fo fofo kutokana na kulewa kupindukia hadi alipokuja kukamatwa
akiwa amelala kwenye kitanda cha Kikongwe akiwa hajitambui.(Picha na
Nathaniel Limu).
Na Nathaniel Limu, Singida
JESHI
la Polisi Mkoa wa Singida linamshikilia mkulima mkazi wa kijiji cha
Wibia tarafa ya Mungaa wilaya ya Ikungi Saidi Hamisi (34) kwa tuhuma ya
kumbaka bibi kizee mwenye umri wa miaka 80 na kumsababishia maumivu
makali katika sehemu zake za siri.
Akizungumza
na waandishi wa habari jana ofisini kwake, kamanda wa jeshi la polisi
mkoa wa Singida, ACP Geofrey Kamwela, alisema tukio hilo la aibu na
kusikitisha limetokea Novemba Sita mwaka huu huko katika kijiji cha
Matongo kata na wilaya ya Ikungi.
Akifafanua,
alisema siku ya tukio mtuhumiwa ambaye alikuwa katika kijiji cha
Matongo kuwajulia ndugu zake hali, alikunywa kiwango kikubwa cha Pombe
ya kienyeji na kupelekea amfanyie kitendo hicho cha kinyama Kikongwe
huyo.
“Mtuhumiwa
alitumia mwanya wa nyumba za Tembe kutokuwa na mlango imara na hivyo
alivuta taratibu mlango uliotengenezwa kwa fito na kuingia mahali
alipokuwa amelala kikongwe huyo. Baada ya kutimiza azma yake, kutokana
na kulewa kupindukia, mtuhumiwa alilala fo fofo huku akikoroma”,alisema.
Kamwela
alisema baada ya kikongwe huyo kubaini kuwa mbaya wake amelala fo fofo
hajitambui, aliweza kutuma wajukuu zake kwenda kutoa taarifa katika
serikali ya kijiji cha Matongo.Viongozi hao waliwasiliana na polisi wa
kituo cha polisi Ikungi kwa simu ambapo walifika haraka, na kumkuta
mtuhumiwa bado anaendelea kuchapa usingizi.
Alisema kwa sasa wanaendelea na upelelezi na utakapokamilika,mtuhumiwa atafikishwa mahakamani kujibu tuhuma inayomkabili.
Katika
hatua nyingine, Kamanda Kamwela ametumia fursa hiyo kutoa wito kwamba
wakazi wa mkoa wa Singida wahakikishe wanakunywa pombe kwa kiwango cha
kawaida na wajihadhari kunywa Pombe kupitiliza kwa madai watashindwa
kufanya maamuzi sahihi.
“Lile
tangazo linalotolewa mara kwa mara na vyombo vya habari kwamba ‘Pombe
ni noma’, lina ukweli mkubwa. Pombe nyingi ina madhara mengi na makubwa
ikiwemo kufikia maamuzi ambayo si sahihi”,alisema.