WANAFUNZI 19 WAFUKUZWA CHUO KIKUU CHA KENYATTA

 Olive Mugenda
Naibu Chansela wa Chuo Kikuu cha Kenyatta Bi Olive Mugenda.

WANAFUNZI 19 wa Chuo Kikuu cha Kenyatta, wametimuliwa chuoni na kutozwa faini kwa kuhusika kwenye maandamano yaliyotokea baada ya kupatikana kwa vifaa vya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka chuoni humo.
Vifaa hivyo vilipatikana na wanafunzi vikiwa vimefungiwa katika kituo cha biashara cha chuo hicho jioni ya Machi 15, ambapo pia palikuwepo maafisa kadha wa IEBC.

Barua nne zilizotumwa kwa wanafunzi hao kuwafahamisha kuhusu hatua zilizochukuliwa zilisema wamefukuzwa kwa mihula miwili, na watahitajika kulipa faini ya Sh30,000 kila mmoja watakaporudi chuoni.

Barua hizo zilizoonekana na Taifa Leo, zilitumwa kwa Mabw Odhiambo Justus Onyango, Omondi Jilali Ochieng, Olweny Steve Rundu na Mathai George Kamau.

“Imeamuliwa kuwa ufukuzwe kwa kipindi cha mihula miwili ili urudi chuoni katika muhula wa kwanza wa mwaka wa 2014/2015. Utahitajika pia kulipa Sh30,000 kugharamia uharibifu uliotokea,” sehemu ya barua hizo ilisema.

Ilisemekana wanafunzi hao walifika mbele ya kamati ya nidhamu Agosti 8, mbali na uchunguzi kufanywa kubainisha ikiwa walihusika.

Uchochezi
Baadhi ya makosa waliyopatikana nayo ni kusababisha ghasia chuoni, kupatikana na vifaa vya IEBC, kuchochea wanafunzi, kuendeleza shughuli za wageni chuoni bila ruhusa na kuzungumzia wanahabari chuoni bila idhini inayostahili.

Tukio hilo lilishuhudiwa wakati kulikuwepo utata kuhusu matokeo ya uchaguzi wa rais, ambapo muungano wa Cord ulikuwa umepinga matokeo ya kutangazwa kwa Uhuru Kenyatta kama mshindi.

Baada ya tukio hilo, IEBC ilitoa taarifa kupinga madai kuwa vifaa hivyo vilikuwa vinatumiwa kubadilisha matokeo ya uchaguzi, na kusisitiza vilitumika katika kura ya mwigo na vilihifadhiwa hapo vikisubiri kupelekwa katika bohari lao.

IEBC pia ililaumu baadhi ya wanasiasa kuchochea wanafunzi hao. Kati ya wanasiasa waliowasili mahali hapo siku hiyo walikuwa Mbunge wa Budalangi Ababu Namwamba, na Millie Odhiambo wa Mbita.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo