WALIOIBA MAHELA YA BENKI YA BACLAYS WAKAMATWA WAKILEWA

WANAUME watatu waliokamatwa mtaani Kawangware Jumapili iliyopita walipodaiwa kulewa baada ya kuvunja benki, Jumatatu walifikishwa mahakamani kujibu mashtaka ya wizi.
Bw Cleophas Musembi, Bw Robert Gikenyi Nyang’au na Bw Charles Kimaiywa walishtakiwa kwa kuvunja tawi la Kawangware la benki ya Barclays, na kuiba takriban Sh330,000 na mtambo wa DVD wa benki hiyo.

Ilidaiwa washukiwa walishirikiana na watu wengine ambao hawakuwa mahakamani kutenda kosa hilo usiku wa Agosti 31 na Septemba 1 mwaka huu.

Bw Musembi na Bw Gikenyi walikabiliwa na shtaka la ziada la kupatikana na mali iliyoshukiwa kuwa ya wizi.

Kulingana na shtaka wawili hao walipatikana na mtambo wa DVD ulioibwa kutoka tawi la Kawangware la benki ya Barclays, na Sh2,900 zilizoshukiwa kuwa sehemu ya zilizoporwa wakati wa kisa hicho.

Mahakama iliambiwa kwamba walipatikana na mtambo huo na pesa hizo nje ya benki hiyo muda mfupi baada ya  majambazi kuvunja na kupora mali usiku wa Agosti 31.

Kila mshukiwa alikanusha mashtaka lakini polisi wakaomba wasiachiliwe kwa dhamana kwa sababu uchunguzi haujakamilika.

Kiongozi wa mashtaka Inspekta Justus Mugambi Imaana aliambia mahakama kwamba polisi walitaka kuwahoji washukiwa kwa siku tatu.

Rumande
Hakimu Mwandamizi wa Kibera Bi Letizia Wachira alikubali ombi lake na kuagiza wazuiliwe katika kituo cha polisi cha Kabete hadi Septemba 4 watakaporudishwa mahakamani.

Mnamo Jumapili, polisi walisema waliwakamata washukiwa watatu waliolewa wakisubiri wenzao kwenye gari nje ya benki ya Barclays mtaani Kawangware wakati wa kisa cha wizi.

Walisema baadhi ya washukiwa waliokuwa ndani ya benki wakitekeleza wizi walifanikiwa kutoroka na kwamba walipata vyombo walivyotumia kuvunja na kuingia katika benki hiyo.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo