MMILIKI WA BASI LILILOSABABISHA AJALI NCHINI KENYA AKAMATWA

 Ajali
MWENYE kampuni ya mabasi ya City to City iliyohusika kwenye ajali katika eneo la Ntulele, Narok, ambapo watu 41 waliuawa Alhamisi iliyopita amekamatwa.
Afisa mkuu wa polisi Narok, Bw Peterson Maelo alithibitisha Jumapili kwamba mfanyabiashara huyo ambaye alijitokeza katika baadhi ya vyombo vya habari wiki jana kutetea kampuni hiyo amekamatwa.

Bw Maelo alisema mfanyabiashara huyo anazuiliwa katika kituo cha polisi cha Muthaiga, Nairobi, na atafikishwa mahakamani Jumatatu.

“Nathibitisha kuwa mmoja wa wamiliki wa kampuni hiyo amezuiliwa katika kituo cha polisi cha Muthaiga na atafikishwa mahakamani kesho asubuhi,” akasema Bw Maelo.

“Tutashtaki kampuni kwa makosa ya kukiuka sheria za trafiki na walionusurika wameandikisha taarifa kuhusu yaliyotendeka,” akasema Bw Maelo.

Lakini alipokuwa akisema hayo, polisi hawakuwa wamemkamata dereva wa basi hilo. Bw Maelo alisema polisi wanafuatilia habari kwamba mshukiwa amelazwa katika hospitali moja ya kibinafsi mjini Kisii na inashukiwa analindwa na watu wakuu serikalini.

“Tunafuatilia habari ambazo bado hatujathibitisha kuhusu dereva wa basi hilo na anayemlinda ili asichukuliwe hatua za kisheria. Tumewasiliana na wenzetu wa Kaunti ya Kisii ili wachunguze madai hayo,” akasema Bw Maelo.

“Nilimuona akishuka kutoka basi hilo. Jamaa zake waliniambia amelazwa katika hospitali moja mjini Kisii,” akasema manusura mmoja aliyeomba tusitaje jina lake.

Wakati huo huo, mili tisa ya waathiriwa wa ajali hiyo ingali katika mochari ya hospitali ya Wilaya ya Narok Kaskazini.

Mkurugenzi wa Afya, Dkt Wago Dulacha, alisema mili 32 tayari imechukuliwa na kusafirishwa hadi Homa Bay kwa mazishi na mingine imepelekwa hospitali tofauti ambapo imehifadhiwa.

Dkt Dulacha alisema kati ya mili tisa ni mmoja pekee uliotambuliwa na wamefanikiwa kutambua jinsi waathiriwa 38 walivyokufa baada ya serikali ya Kaunti ya Narok kulipa ada ya Sh5,000 iliyohitajika.

Akizungumza na wanahabari nje ya hospitali hiyo, Dkt Dulacha alisema manusura watano, akiwemo mtoto mmoja na wanawake wanne bado wamelazwa hospitalini.

“Bado wanatibiwa kabla ya kuruhusiwa kwenda nyumbani. Wengi wao wana majeraha mabaya,” akaongeza.

Manusura
Alisema wote waliojeruhiwa wako katika hali thabiti na wataruhusiwa kwenda nyumbani hivi karibuni.

Alisema kufuatia ajali hiyo ya Alhamisi, manusura 32 walihamishwa hadi Hospitali Kuu ya Kenyatta, Nairobi, ambako mmoja alifariki na kuongezea idadi ya waliofariki kufikia 42.

“Waliohamishwa hadi Kenyatta walikuwa na majeraha ya kichwa na wanahitaji uchunguzi maalumu na hospitali hii haina vifaa vinavyohitajika,” akasema Dkt Dulacha.

Millie Akinyi, 20, ambaye alikuwa abiria katika gari hilo, alisema ni muujiza kwamba yeye na mtoto wake mwenye miaka miwili walinusurika wakati wa ajali hiyo. Bi Akinyi alipata majeraha madogo huku bintiye akikwaruzwa usoni.

Na JOYCE BOKE Na GEORGE SAYAGIE


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo