WAANDISHI WA HABARI WAGOMEA KUINGIA KWENYE CHUMBA WALICHOPANGIWA KWENDA KUCHUKUA HABARI


  Mbunge wa Dujis Aden Duale
Bw Aden Duale akihutubia wanahabari awali

Na ISAAC ONGIRI
WANAHABARI zaidi ya 30 nchini Kenya leo wamezua kioja katika majengo ya Bunge walipokataa kuchukua taarifa ya Kiongozi wa Wengi Bungeni, Bw Aden Duale.
Wanahabari hao ambao walikuwa wamekusanyika bungeni walikataa kuripoti kuhusu mkutano huo wakipinga kutimuliwa kwao katika chumba kilichotengewa wanahabari katika majengo hayo miezi kadha iliyopita na wasimamizi.

Bw Duale na wabunge zaidi ya 15 wa muungano wa Jubilee walikuwa tayari wameketi katika chumba hicho kinachotambuliwa kama cha wanahabari bungeni, huku wakiwasubiri wanahabari hao kupanga vifaa vyao, lakini walipata mshtuko wanahabari hao walipokataa kuingia mahali hapo.

Mbunge huyo wa  Garissa Mjini na mwenzake wa Othaya Mary Wambui walitoka nje kuwasihi wanahabari kuchukua taarifa yao lakini hawakufua dafu.

“Tumeomba mje mchukue taarifa yetu. Tumekusanyika hapa na mimi ndio nimewaita kwa hivyo, tafadhalini ingieni mchukue taarifa,” alisema Bw Duale. Lakini wanahabari hao walisisitiza kuwa wanaweza tu kuchukua taarifa ya Bw Duale na wenzake nje ya majengo hayo ili kufuata agizo lililotolewa na Spika wa Bunge la Kitaifa, Bw Justin Muturi.

“Agizo la Spika kuzuia kufikia chumba cha wanahabari bado halijaondolewa. Ikiwa hilo limefanyika basi mawasiliano rasmi bado hayajafanyika. Tafadhali, huenda ikaonekana kana kwamba tunaingia bila idhini kwa sisi kuendesha shughuli katika kituo cha wanahabari,” mmoja wa wanahabari alimueleza Bw Duale.

Bi Wambui aliomba suala hilo linalozua utata kati ya umma na bunge litatuliwe kwa haraka.

Ulinzi
“Hili ni suala rahisi. Linastahili kutatuliwa haraka iwezekanavyo lakini kwa sasa njoni mchukue taarifa yetu,” alisema.

Baadaye, kundi lingine la wabunge 11 wa jamii ya Maa  likiongozwa na  mbunge wa Kajiado Magharibi Moses Ole Sakuda pia walikusanyika mahali papo hapo na kuwauliza wanahabari wachukue taarifa yao. Lakini wanahabari hao pia walimuuliza Bw Sakuda na wenzake kuwahutubia wakiwa nje ya majengo ya bunge wakitoa sababu zile zile.

“La, hatuwezi kuwahutubia kutoka nje ya bunge kwa sababu baadhi ya masuala tulitaka kujadili ni mazito na yanahitaji ulinzi wa bunge,” alisema Bw Sakuda.

Miezi miwili iliyopita Spika wa Bunge aliagiza kituo hicho cha wanahabari kifungwe na kompyuta zilizokuwa hapo ndani  kuondolewa ili vyumba hivyo viwili vilivyokuwa awali vimetengewa wanahabari, viweze kutumiwa sasa na kamati za bunge.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo