WAALIMU NCHINI KENYA WATISHIA KUGOMA TENA

Wilson Sossion
Mwenyekiti wa Chama cha Kitaifa cha Walimu (KNUT) Wilson Sossion. 

CHAMA cha Kitaifa cha Walimu (Knut) kimetishia kuitisha mgomo mwingine iwapo walimu hawatalipwa mishahara yao ya Julai.
Viongozi wa chama hicho wamesema tayari wamewasilisha ilani kwa serikali, na watachukua hatua Jumanne ijayo bila kutoa ilani nyingine yoyote.

Kwenye kikao na wanahabari katika afisi za Knut Nairobi, Katibu Mkuu wa chama hicho Mudzo Nzili, amesema serikali imedhihirisha haiwezi kuaminika, kwa kuwa imeenda kinyume na makubaliano yao yaliyopelekea kusitishwa kwa mgomo uliodumu kwa siku 24.

“Tuliweka makubaliano ya kurejea kazini na mwajiri, na yalishuhudiwa na waziri wa leba pamoja na wakuu wengine wa serikali. Makubaliano lazima yaheshimiwe na pande zote mbili za mwajiri na mwajiriwa,” alisema.

Kulingana na Bw Nzili, walimu walikubali kuongeza muda wa muhula ili kujaza kipindi kilichopotezwa wakati wa mgomo, huku TSC ikikubali kuwa walimu hawataadhibiwa kwa kuhusika kwenye mgomo.

Uamuzi wa TSC kutolipa walimu waliohusika kwenye mgomo ulitokana na pendekezo lililowasilishwa kwao na Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC), iliyodai si haki kwa mfanyakazi kulipwa ilhali hakufanya kazi anayolipiwa.

Bw Nzili alisema inashangaza kuwa serikali ilikubali kuwalipa tu marupurupu ya Sh11.5 bilioni kwa awami ya miaka mitatu, ilhali inataka kuchukua Sh13bn ambayo walimu wangelipwa mwezi huu.

Chama hicho pia kilisema TSC imekiuka sheria kwa kuchukua hatua hiyo, kwani makubaliano yao yalisajiliwa katika Mahakama ya Viwanda ambayo sasa ina mamlaka ya kusimamia utekelezaji wake.

Isitoshe, mwenyekiti wa Knut Wilson Sossion, aliongeza tume hiyo imekiuka sera zake za uadilifu kuhusu jinsi ya kuadhibu utovu wa maadili.

Kulingana na Bw Sossion, walimu wanaolengwa kuadhibiwa wangepewa nafasi ya kujitetea kabla hatua yoyote kuchukuliwa dhidi yao.

“Hakuna mwalimu aliyesikizwa, ilhali TSC imechukua hatua ya kukata mishahara yao. Tunashangaa walichukua hatua hii kwa msingi gani,” alisema.

Septemba
Huku shule zikitarajiwa kufungwa Agosti 16, Bw Sossion alisema wanaweza kugoma hadi Septemba ikiwa hilo litahitajika.

“Walimu ni binadamu na hawana mbinu nyingine ya kujipatia riziki, na huku tuko na serikali ambayo ni mbaya zaidi ya ile ya mkoloni na zingine zilizotangulia,” alisema Bw Sossion.

Kamati ya Ushauri ya chama hicho ambayo ndiyo kuu zaidi, inayojumuisha wanachama 500 kutoka kila tawi nchini, inapangiwa kukutana Jumatatu na kuamua hatua itakayochukuliwa.
 
Bw Sossion alisema hawatashtushwa na kufungiwa gerezani, ikiwa hiyo itapelekea walimu kutendewa haki.


JIUNGE NA EDMO BLOG SASA

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia Facebook,Twitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga na Youtube kuangalia video zote kali kutoka Edmo Blog Pekee!, kujiunga bonyeza hapa>>>Youtube

Tupe Maoni Yako lakini Usiandike Matusi



 
© Copyright EDMO BLOG | Designed By Peruzibongo